Sibuka FM
Sibuka FM
17 March 2026, 1:22 pm

“Ni kweli hakuna mtu asiyependa maendeleo ya nchi yake kila wananchi anatamani kuona miradi ya maendeleo inatekelezwa kwa wingi bila changamoto zozote zile za kimaslahi kwa wale wanaopaswa kulipwa fidia zao kutokana na kupisha miradi hiyo katika maeneo hayo”.
Na,Daniel Manyanga
Mkuu wa mkoa wa Simiyu Anamringi Macha amesema kuwa serikali ya mkoa huo itaendelea kusimamia na kuhakikisha wananchi wake wanapata haki sawa kwenye maeneo yao yanayochukuliwa kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo ili kuondoa migogoro ya ardhi hasa kwa wamiliki wa maeneo hayo.
Anamringi Macha ameyasema hayo wakati akipokea ripoti ya uthamini ardhi wa mara ya pili uliofanyika kwa ajili ya kutatua mgogoro wa fidia uliokuwepo kati ya chuo cha usimamizi wa fedha na mipango (IFM) kampasi ya Simiyu, na wananchi wa kijiji cha Sapiwi ambao walikuwa wamegomea fidia ya awali wakidai kuwa ilikuwa haiendani na thamani ya ardhi iliyochukuliwa na chuo hicho kwa ajili ya ujenzi wa chuo.
Silas Honga ni mthamini mwandamizi wa ardhi ambaye pia ni mwenyekiti wa kamati ya utatuzi wa mgogoro huo ameeleza matokeo ya uthamini huo wa mara ya pili huku mkuu wa idara ya mipango na maendeleo wa chuo hicho Dkt. Ezra Kakozi akisema kuwa fedha hizo zitalipwa kwa wahusika kwa wakati mwafaka.
Songolo Mayuma, Suleiman Mayongela na Emmanuel Maseko ni baadhi ya wananchi waliokuwa wamegomea fidia ya awali wamesema kuwa wamekubaliana na uthamini huo wa mara ya pili na kwamba wako tayari kupokea fidia itakayotolewa kwa sasa.