Sibuka FM
Sibuka FM
6 March 2026, 9:27 am

“Tunatumia nguvu kazi kubwa sana hadi pamba kufika sokoni tukitarajia tutapata faida kutokana na kile ambacho tumekifanya kwa msimu mzima wa kilimo halafu panatokea mtu mmoja tu anaanza kutengeneza faida kutokana na jasho la watu wengine hii haipo sawa tunawavunja moyo wakulima wetu”.
Na,Daniel Manyanga
Wakulima wa zao la pamba mkoani Simiyu wameiomba serikali ya mkoa kuwashughulikia wanunuzi wa pamba waliofanya udanganyifu msimu wa mwaka jana wa kuwaibia wakulima wakati wa mauzo kg 20 kwenye kila kg 100 baada wa wanunuzi hao kuchezea mizani.
Julai mwaka jana wakala wa vipimo mkoani hapa walifanya oparesheni ya kushtukiza na kubaini uwepo wa mizani iliyochezewa na baadhi ya watu waliokutwa walikimbia na katika oparesheni hiyo jumla ya mizani 180 ilikaguliwa na 60 ilikutwa imechezewa na kufatia sakata hilo la baadhi ya wahusika kujulikana na hatua kali za kisheria zimeanza kutekelezwa kwa wale wote waliohusika kuwaibia wakulima wa zao la pamba.
Wakizungumza na SibukaFm,George Heke,Emmanuel Myembela na Paulo Makalanga ambao ni wakulima wa pamba kupitia viongozi wao wameiomba serikali kuwachukulia hatua wahusika wote ili iwe fundisho kwa wanaotaka kuendelea na mchezo huo kabla ya msimu mpya wa manunuzi kuanza ili kuleta tija kwa wakulima hao kutokana na kazi ngumu wanayoifanya ya kilimo hicho.
Kwa upande wake mkuu wa mkoa wa Simiyu, Anamringi Macha amesema msimu uliopitia jambo lililowasumbua wakulima wa pamba mkoani hapa baada ya msimu wa uuzaji wa pamba kufunguliwa ni baadhi ya watu wasiokuwa waaminifu kuchezea mizani hali iliyopelekea kutofikia matarajio ya mauzo waliyoyakusudia hivyo msimu huu haitatokea na lazima sheria kali zichukuliwe kwa wale wote waliobainika kufanya mchezo huo mchafu kwa wakulima wa pamba.