Sibuka FM
Sibuka FM
3 February 2026, 9:09 am

Utawala wa sheria ndio nguzo muhimu katika kuleta Ustawi na Maendeleo kwa Nchi, hivyo Mahakama ina mchango mkubwa ” Enos Missana
Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Maswa, Mkoani Simiyu imeunda kamati maalumu kwa ajili ya kusikiliza na kutatua kero na Migogoro mbalimbali ili kusaidia wananchi kupata haki zao za msingi kwa urahisi ambapo kila Alhamisi ya wiki imekuwa ikisikiliza migogoro na malalamiko ya wananchi
Akizungumza katika Sherehe ya siku ya Sheria Nchini, Katibu tawala Wilaya ya Maswa ndugu Athuman Kalaghe akimuwakilisha Mkuu wa Wilaya hiyo Dkt Vicent Naano Anney amesema kuwa kuanzishwa kwa kamati hiyo kutasaidia kuleta ustawi kwa Wananchi huku akitoa pongezi nyingi kwa Mahakama za Maswa kwa kusimamia Haki vizuri hali inayofanya malalamiko ya wananchi kupungua
Kwa upande wake Hakimu Mkazi Mfawidhi Mkahakama ya wilaya ya Maswa Mhe Enos Missana ambae alikuwa Mgeni rasmi katika sherehi hiyo amesema kuwa utawala bora ndio nguzo muhimu katika kuleta Ustawi na Maendeleo kwa Nchi kwani Mahakama ndio chombo kinachotofasri sheria, kulinda haki za binadamu na kuhakikisha hamna mtu aliye juu ya sheria
Aidha Mhe Missana ametoa wito wa wadau wa sheria kushirikiana na mahakama ili kufikia malengo endelevu na ustawi wa Taifa hivyo bila kuwa sheria bora hakuna utaratibu bora wa kijamii

Suzan Masule ni mwendesha mashtaka kutoka Ofisi ya Taifa ya mashtaka wilaya ya Maswa amesema kuwa ili mahaama iweze kutoa mchango katika ustawi na Maendeleo ya Nchini ni lazima mahakama iwe huru kutoka kwenye ushawishi , Msukumo au vitisho kutoka muhimili mwingine
Naye Daudi Masunga kutoka Chama cha Wanasheria Tanganyika – TLS amesema kuwa wataendelea kutoa ushauri wa kitaaluma kwenye mabadiliko na marekebisho ya sheria mbalimbali huku akiipongeza mahakama kwa maboresho ya makubwa ya mifumo ya uendeshaji wa mashauri kupitia mfumo wa Tehama

