Sibuka FM
Sibuka FM
29 May 2025, 12:19 pm

‘‘Ni kweli bado jamii yetu inakabiliwa na changamoto mbalimbali zipo familia zenye uwezo wa kiuchumi lakini hizi ambazo hazina uwezo wa kimaisha tunawezaje kuzisaidia ili nazo ziweze kupata furaha hili ni jambo tunaweza kulifanya tu endapo watu wenye uwezo mkubwa kiuchumi wenye moyo wa kusaidia watu wafanya hivyo kadri wawezavyo’’.
Na,Daniel Manyanga
Jamii wilayani Bariadi mkoani Simiyu imeshauriwa kujijengea tabia ya kuwakumbuka watu wenye mahitaji mbalimbali kwa kuwatembelea na kuwasadia ili kuwawezesha kuondokana na changamoto zinazowakabili sawasawa na maandiko matakatifu yanayotoka kwenye vitabu vitakatifu vya Mungu ya kwamba dini ya kweli ni kuwakumbuka au kuwajali wenye uhitaji.
Ushauri huo umetolewa na vijana wa UVCCM wilaya ya Bariadi Isaac Nzige, Magreth Jumanne na Benjamin Omary, walipotembelea na kutoa misaada mbalimbali kwa wagonjwa waliolazwa katika hospitali ya halmashauri ya mji wa Bariadi, ikiwemo akinamama waliojifungua na wanaotarajiwa kujifungua pamoja na watoto wanaoendelea kupatiwa matibabu hospitalini hapo na kueleza umuhimu wa jamii kuendelea kuwakumbua watu wenye uhitaji.
Omary Mohammed ni muuguzi mfawidhi wa hospitali hiyo ya halmashuari ya mji wa Bariadi, amewakumbusha vijana na jamii kiujumla yenye uwezo kipato kuendelea kuwasaidia wagonjwa na watu wengine wenye uhitaji waliopo kwenye jamii zetu.

Kwa upande wao Tumaini Mtawala, Salome Elias na Mary Masunga ambao ni baadhi ya wagonjwa waliopatiwa misaada hiyo wameeleza itakavyowasaidia kipindi ambacho bado wapo hospitalini wakiendelea kupatiwa matibabu hivyo wameiomba jamii iendelee kuwa na moyo wa huruma wa kuwaona hata watu wasio na uwezo wanaohangaika kila siku kutokana na changamoto za kimaisha.
