Sengerema FM
Sengerema FM
6 June 2026, 12:20 pm

Kutokana na kukithili kwa vitendo vya ukatili dhidi ya watoto nchini, Afisa Tarafa ya Katunguru wilayani Sengerema Kibasa Samwel Masangwa ameitaka jamii kushirikiana na serikali ili kukomesha vitendo hivyo.
Na, Emmanuel Twimanye
Watoto Wilayani Sengerema mkoani Mwanza wameiomba serikali kuchukua hatua madhubuti za kukomesha vitendo vya ukatili dhidi ya watoto ikiwa ni pamoja na kuwachukulia hatua za kisheria wahusika wa vitendo hivyo.
Hayo yamesemwa na watoto hao katika maadhimisho ya Siku ya Mtoto wa Afrika yaliyofanyika kiwilaya katika Kata ya Nyamizeze Wilayani Sengerema ambapo wamesema vitendo vya ukatili bado vinaendelea katika baadhi ya maeneo na vinakwamisha haki zao za msingi.
Baadhi ya viongozi wa serikali za mitaa wameahidi kuendelea kufichua matukio ya ukatili dhidi ya watoto ili wahusika wachukuliwe hatua za kisheria.
Akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa Wilaya ya Sengerema Mh, Senyi Ngaga, Afisa Tarafa ya Katunguru Kibasa Samwel Masangwa ameitaka jamii kushirikiana na serikali katika kupinga vitendo vya ukatili na unyanyasaji dhidi ya watoto.
Kwa upande wake, Afisa Maendeleo ya Jamii wa Halmashauri ya Wilaya ya Sengerema, Yuster Mwambembe ameahidi kutekeleza maelekezo yaliyotolewa na Afisa Tarafa ya Katunguru ili kusaidia kukomesha vitendo hivyo.
Aidha, Maadhimisho ya Kimataifa ya Siku ya Mtoto wa Afrika yanatarajiwa kufanyika Juni 16 mwaka huu yakiwa na kaulimbiu isemayo, “Mtoto ni Malezi; Msingi wa Familia Bora kwa Taifa Imara.”


