Sengerema FM

Marufuku kwenda na watoto kwenye kumbi za Starehe

4 April 2024, 4:26 pm

Mwenyekiti wa Mtaa wa Migombani Mjini Sengerema Anton Busumabu akizungumza akiwa Ofisini kwake. Picha na Emmanuel Twimanye

Kutokana na kkuongezeka kwa mmomonyoko wa maadili kwa watoto nchini Serikali ya mtaa wa Migombani Imepiga marufuku wazazi kwenda na watoto kwenye kumbi za Starehe mjini Sengerema

Na:Emmanuel Twimanye

Serikali ya mtaa wa Migombani Kata ya Nyampulukano Wilayani Sengerema Mkoani Mwanza imepiga marufuku wazazi kwenda na watoto sehemu za starehe ili kuepuka wimbi la mmomonyoko wa maadili kwa watoto.

Marufuku hiyo imetolewa na Mwenyekiti wa mtaa wa Migombani  Anton Busumabu kufuatia kukithiri kwa baadhi ya wazazi kwenda na watoto wao sehemu za starehe na kuahidi kuwachukulia hatua kali za kisheria  wazazi watakaokaidi agizo hilo.

Sauti ya Mwenyekiti wa mtaa wa Migombani  Anton Busumabu akizungumzia kuwachukulia hatua wazazi watakao kaidi

Katika hatua nyingine mwenyekiti huyo ameyataka  baadhi ya makanisa yanayopiga muziki kwa sauti ya juu  kuacha mara moja, kwa kuwa yanapelekea usumbufu kwa wakazi  wanaoishi karibu na makanisa hayo. 

Sauti ya Mwenyekiti wa mtaa wa Migombani  Anton Busumabu akizungumzia baadhi ya makanisa kupiga muziki

Mhudumu wa afya ngazi ya jamii  Raheli Faustine  amesema kuwa watoto  wengi  wamekuwa   wakikutana  nao  kwenye  baa wakati wakitoa elimu ya kujikinga na ugonjwa wa kipindupindu  hali ambayo  inahatarisha  maadili ya watoto.

Sauti ya Mhudumu wa afya ngazi ya jamii  Raheli Faustine

Nao baadhi ya wananchi wa mtaa huo wameiomba serikali kuwachukulia hatua kali za kisheria wazazi watakaobainika kwenda na watoto baa kwa kuwa ni chanzo cha mmomonyoko wa maadili kwa watoto.

Sauti ya Wananchi wa mtaa wa Mgombani

Naye Shekhe wa wilaya ya Sengerema ambaye pia ni mwenyekiti wa kamati ya Amani wilayani humo Shekhe Ahmad Jah  amekemea  tabia hiyo   kwani   inaharibu maadili ya watoto.

Sauti ya Sheikh wa Wilaya ya Sengerema Shekhe Ahmad Jah 

Aidha suala la baadhi ya wazazi  kwenda na watoto sehemu za starehe  limeshika kasi  wilayani Sengerema  licha ya  Sheria ya mtoto ya  mwaka 2009  kuzuia  jambo hilo.