Sengerema FM
Sengerema FM
16 June 2026, 7:04 pm

Baada ya baadhi ya watoto kuwa na tabia za wizi na udokozi wa vitu vya nyumabani, mama mmoja ameiomba serikali kumchukulia hatua za kisheria binti yake kwa wizi wa mahindi ili iwe fundisho kwa wengine.
Na, Emmanuel Twimanye
Binti aliyefahamika kwa jina la Sauda Selemani Mkazi wa mtaa wa Igogo Kata ya Nyampulukano Wilayani Sengerema Mkoani Mwanza amekamatwa kwa tuhuma za wizi wa mahindi.
Akizungumzia tukio hilo binti huyo akiwa chini ya ulinzi wa polisi jamii amekiri kuiba mahindi kiasi cha debe mbili na kwenda kuyauza.
Mama aliyeibiwa mahindi ambaye pia ni mama mzazi wa binti huyo Salah Isack amesikitishwa na tukio hilo na kuiomba serikali kumchukulia hatua kali za kisheria binti huyo ili liwe fundisho kwa watu wengine wenye tabia hiyo.
Baadhi ya ndugu na majirani wamesikitishwa na kitendo cha binti huyo cha kujihusisha na wizi na kuwaomba mabinti kuachana na vitendo hivyo.
Kamanda wa polisi jamii kata ya Nyampulukano Lenatus Lugadija amethibitisha kukamatwa kwa binti huyo kwa tuhuma za wizi wa mahindi na kuahidi kumfikisha kwewnye vyombo vya dola kwa hatua zaidi za kisheria.
Kwa upande wake ,Mwenyekiti wa mtaa wa Igogo Goodluck Daud amewataka wazazi na walezi kuwa makini na watoto ikiwa ni pamoja na kuwashauri kuacha wizi ili kuepuka kuhatarisha maisha yao.