Chai FM

MKURABITA yaja na mpango kwa wafanyabiashara Rungwe

12 May 2022, 1:03 pm

RUNGWE-MBEYA

Mpango wa kurasimisha rasirimali na biashara Tanzania (MKURABITA) umekuja na mpango wenye lengo kuwawezesha wamiliki wote wenye biashara nje ya mfumo rasmi ili waweze kurasimishwa Wilayani Rungwe hali itakayo saidia kupata mitaji na kuendeleza shughuli zao za kiuchumi.

Hayo yamesemwa na Jane Lyimo  Mkurugenzi wa Urasimishaji ardhi na biashara Mkurabita amesema mpango huo utatoa mafunzo kwa wafanyabiashara  takribani elfu mbili ya urasimishaji kwa kuanza na Kata kumi na moja Wilayani Rungwe.

Aidha Lyimo amesema mafunzo hayo yatajumuisha wadau kutoka ofisi ya biashara, mamlaka ya mapato Tanzania(TRA),Taasisi za fedha,NSSF ,TCCIA na SIDO kwaajili ya kusaidia kundi la wafanyabiashara watakaoudhuria katika mafunzo hayo.

Sambamba na hayo amewataka wafanyabiashara kuudhuria mafunzo hayo yatakayotolewa bure ili kuendesha biashara endelevu na kuinuka kiuchumi.