Sibuka FM

Maswa: Zaidi ya wananchi laki mbili wamepata chanjo ya covid-19

18 May 2023, 4:16 pm

Kwenye ni mkuu wa kitengo cha Usafi na Mazingira wilaya ya Maswa ,Budodi Walwa akimpatia chanjo ya Covid-19 mmoja wa wananchi wilayani hapo

Na Alex.F.Sayi.

Zaidi ya Wananchi laki  mbili Wilayani Maswa Mkoani Simiyu  wamepata chanjo ya Covid-19 kufuatia mpango wa halmashauri kwa kushirikiana na wadau wa afya mpaka mwezi December mwaka jana.

Hayo yamesemwa na  mratibu wa chanjo  Wilaya ya Maswa, Abel Machibya ,ambapo amesema kuwa Halmashauri ya Wilaya wamechanja kwa 102% nakuvuka lengo walilopangiwa na Serikali hali iliyosaidia kupunguza kwa kiasi kikubwa kasi ya  maambukizi ya Ugonjwa huo Wilayani hapa.

Machibya ameongeza kuwa idadi hiyo ya wananchi kupatiwa chanjo ya Covid-19 iliongezeka kufuatia uwepo wa vipindi vya elimu ya chanjo kupitia Sibuka Fm hali ambayo imewezesha kufikiwa kwa wananchi kwa urahisi na kuweza kuchanja zaidi ya wananchi laki mbili wilayani hapa.

“Uwepo wa wadau wa Afya Internews na Tadio wamechanjia sehemu kubwa sana katika kufikisha elimu hii kwa wananchi wetu ambao wengi wao walikuwa wakisita kupata chanjo hii kutokana na kutokuwa na imani na chanjo hii’’.Amesema Machibya.

“Mpaka december mwaka jana halmashauri ya wilaya ya Maswa tulikuwa na wananchi 221,224 walipata chanjo lakini kuanzia mwezi Jnuary hadi April halmashauri kwa kushirikiana na Sibuka fm kupitia vipindi vya afya tumefanikiwa kuongeza idadi ya wananchi kupata chanjo hii ,lakini bado halmashauri tunaandaa kampeni nyingine na hii itawafikia wananchi wengi zaidi’’.Amesema Machibya

Modesta Ndamo ,ni Mkazi wa Mjini Maswa mwenye Umri wa miaka (76)  akizungumzia uzoefu  alioupata kwa  mwaka mmoja sasa toka apate chanjo ya Covid-19 amesema kuwa  hali ya Afya yake kwa sasa  inaendelea vizuri na hajapata shida yoyote ile  kiafya tangu achanje Chanjo hiyo ya Covid 19 mwaka mmoja uliopita.

“Kumekuwepo na taarifa nyingi sana huku kwenye jamii yetu ambazo hazina ukweli wowote juu ya chanjo ya Covid-19 wengi wakidai ni mpango wa Wazungu kuimaliza Afrika,mimi nilipopata chanjo hii nililazimika kujificha nikiogopa kuchekwa na jamii lakini elimu ya mara kwa mara imenisaidia sana kujiamini ’’ .Amesema Ndamo

“Mwanzoni kabisa Corona inaingia hapa nchini hakukuwa na elimu ya kutosha kwa wananchi lakini tuwashukuru sana wadau wa afya kupitia Sibuka fm imenifanya nipate chanjo baada ya kuwa na uelewa zaidi juu ya chanjo hii’’. Amesema Issa Mathias