Karagwe FM

Missenyi na Maendeleo yachangia madawati 85 kwa wanafunzi 255

18 September 2026, 20:02

Picha ya pamoja na mgeni rasmi mkuu wa wilaya ya Missenyi Kanali Mstaafu Hamis Mayamba Maiga (mwenye kofia). Picha na Mwandishi wetu

Tatizo la upungufu wa madawati limekuwa likijitokeza kote nchini kila mwaka hasa nyakati za uandikishaji wa wanafunzi wa darasa la awali na la kwanza kwa shule za msingi sambamba na uandikishaji wa kidato cha kwanza kwa shule za sekondari.

Na Mwandishi wetu, Missenyi

Kikundi cha mtandaoni (WhatsApp) cha Missenyi na Maendeleo kimekabidhi mchango wa madawati 85 yenye thamani ya shilingi milioni 5.1 kwa mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya Missenyi

Madawati hayo yamekabidhiwa Septemba 17.2026 baada ya kuchangwa na wanagroup wazalendo wa kikundi cha mtandao wa WhatsApp cha Missenyi na Maendeleo ili kupunguza tatizo la upungufu wa madawati katika shule za msingi na sekondari wilayani humo

Mgeni rasmi katika hafla ya kukabidhi madawati hayo amekuwa mkuu wa wilaya ya Missenyi Kanali Mstaafu Hamis Mayamba Maiga akishuhudia shule nne za msingi zikipata mgao wa madawati 85 kama zilivyotajwa na kaimu mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya Missenyi Seraphina Rwegasira

kaimu mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya Missenyi Seraphina Rwegasira
Mwl mkuu wa shule ya msingi Omurugando akipokea madawati 30 yanayokidhi mahitaji ya shule yake. Picha na Mwandishi wetu

Mratibu na kiongozi wa kikundi hicho bw. Respicius John amesema kuwa kikundi hicho kilianzishwa Agosti 21. 2020 kikihusisha wadau wa maendeleo na kwamba wazo la uchangiaji madawati lilianzishwa mwaka huu na mmoja wa wadau hao kisha utafiti ukabaini uhitaji wa kutekeleza jambo hilo kupitia michango ya hiari

Amesema kuwa kipaumbele cha mgao wa madawati umezingatia shule zilizokuwa na uhitaji mkubwa wa samani hizo huku akitaja mikakati ya kikundi hicho kwa siku zijazo

Sauti ya mratibu na kiongozi wa kikundi cha WhatsApp “Missenyi na Maendeleo” bw. Respicius John

Naye mgeni rasmi mkuu wa wilaya ya Missenyi Kanali mstaafu Hamis Maiga ameitaka jamii ya Missenyi kuunga mkono juhudi zinazofanywa na wadau hao huku akiwataka walimu wa shule zilizonufaika kutunza samani walizozipokea

Pia amewaagiza walimu wakuu kuanzisha utaratibu na ratiba ya kurekebisha samani zinazoharibika ili kuzuia upungufu mkubwa wa madawati shuleni

Sauti ya mkuu wa wilaya ya Missenyi Kanali mstaafu Hamis Maiga
Baadhi ya walimu wa shule za msingi zilizopata mgao wa madawati wakifurahia tatizo la upungufu wa madawati kutatuliwa katika shule zao. Picha na Mwandishi wetu

Hata hivyo kwa mujibu wa kaimu mkurugenzi wa halmashauri hiyo bado kuna upungufu wa madawati 1,916

Ameiomba jamii na wadau wa maendeleo kuendelea na juhudi za uchangiaji wa madawati ili kumaliza kabisa tatizo la upungufu na kuweka mazingira bora ya wanafunzi kujifunza