Karagwe FM

Ulaji wa vyakula vya mafuta na wanga bila mazoezi ni chanzo cha magonjwa yasiyoambukiza

14 November 2023, 12:56 pm

Magonjwa yasiyokuwa ya kuambukizwa ni magonjwa anayoweza kuyapata mtu yeyote bila kuambukiza watu wengine

Na: Shabani Ngarama, Karagwe

Mtangazaji wa Kipindi cha Dira ya Leo Radio Karagwe bi Ospicia Didace, akiongoza kipindi na Daktari Jaspa. Picha na: Shabani Ngarama

Imeelezwa kuwa chanzo kikubwa cha magonjwa yasiyoambukiza kwa wananchi wa wilaya ya Karagwe ni ulaji mbaya wa vyakula vya mafuta na wanga, kula bila mpangilio bila kuwa na ratiba ya kufanya mazoezi. Akiongea na Radio Karagwe katika kipindi cha Dira ya leo Novemba 14,2023 mratibu wa huduma za afya na magonjwa yasiyokuwa ya kuambukiza wilaya ya Karagwe Dk. Ntongani Jaspa amesema kuwa magonjwa yasiyokuwa ya kuambukizwa ni magonjwa anayoweza kuyapata mtu yeyote bila kuambukiza watu wengine. Amenukuu jarida la shirika la afya duniani WH0 la tarehe 16 Septemba mwaka huu akisema kuwa watu milioni 41 hufariki dunia kwa mwaka mmoja kutokana na magonjwa haya na kwamba asilimia 74 vifo vyote duniani husababishwa na magonjwa yasiyo ya kuambukiza

Mratibu wa huduma za afya na magonjwa yasiyoambukiza wilaya ya Karagwe Daktari Ntongani Jaspa.

Na, Shabani Ngarama

Ameyataja magonjwa sumbufu kwa jamii yasiyokuwa ya kuambukiza kuwa ni pamoja na Kansa, Kisukari,Selimundu,magonjwa ya mfumo wa hewa, magonjwa ya afya ya akili na ajali. Dk Ntongani amewataka wananchi kuzingatia ratiba ya ulaji na kuepuka matumizi ya vyakula vya mafuta na wanga kwa wingi ili kuepuka magonjwa haya. Hata hivyo amewashauri wananchi kuweka ratiba ya mazoezi ili kupunguza mafuta mwilini na iwapo watabainika kupata magonjwa haya watibiwe kwa usahihi ili kuepuka ugonjwa wa kiharusi.

Sauti ya mratibu wa huduma za afya na magojwa yasiyokuwa ya kuambukiza Daktari Ntongani Jaspa

Itakumbukwa kuwa Novemba 10 hadi 16 dunia haudhimisha wiki ya mahonjwa yasiyoambukiza ambapo serikali ya Tanzania kupitia idara ya afya hutumia wiki hii kuelimisha jamii juu ya mambo muhimu ya kuzingatiwa kwa watu ili kuepuka magonjwa haya sambamba na namna ya kuishi kwa usalama kwa waliokwishaathirika na magonjwa haya