Karagwe FM
Karagwe FM
13 May 2026, 13:41

Halmashauri ya Karagwe mkoani Kagera imeendelea kuwekeza katika miundombinu ambapo sasa wanakuja na mradi wa kimkakati wa soko la kisasa.
Na Jovinus Ezekiel, Karagwe
Halmashauri ya wilaya Karagwe mkoani Kagera inatarajia kuanza utekelezaji wa mradi wa ujenzi wa soko la kisasa litakalojengwa kwa fedha za serikali kuu kwa lengo la kukuza uchumi wa wananchi.
Hayo yameelezwa na mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya wilaya ya Karagwe Happines Msanga Mei 12. 2026 katika ukumbi wa halmashauri hiyo Angaza mjini Kayanga wakati akizungumza na wajumbe wa kikao cha baraza la mamlaka ya mji mdogo wa Kayanga na kuongeza kuwa soko hilo litajengwa kwa fedha za serikali kuu na kwamba tayari shilingi bilioni 1 zimetengwa kwa ajili ya kuanza ujenzi

Mwenyekiti wa halmashauri ya wilaya ya Karagwe Longino Wilbard Rwenduru (wa kwanza kushoto) akiwa katika kikao cha baraza la mamlaka ya mji mdogo wa Kayanga. Picha na Jovinus Ezekiel
Baadhi ya wajumbe wa mkutano huo akiwemo mwenyekiti wa kitongoji cha Kagururu Josephina Bitekelelo, Samson Wilson China wa Omugakorongo na Gidion Machage wa kitongoji cha Bomani wameishukuru serikali kwa kubuni mradi huo wakieleza kuwa utakuwa chachu ya ukuaji wa uchumi wa Karagwe

Mwenyekiti wa halmashauri ya wilaya ya Karagwe na diwani wa kata ya Chanika Longino Wilbard Rwenduru amewashukuru wenyeviti wa vitongoji vinavyounda mamlaka ya mji mdogo wa Kayanga kwa jinsi wanavyoendelea kuchapa kazi sambamba na kuwataka kudumisha mshikamano. Hata hivyo mwenyekiti wa mamlaka ya mji mdogo wa Kayanga na mwenyekiti wa kitongoji cha Katooma Ruzinga Projest Kajuna amesifu hatua ya serikali kuanzisha mradi huo