Wananchi watumia maji ya madimbwi kwa miaka 60 Bweyaja
5 May 2024, 4:48 pm
Kitongoji Bweyaja kina tatizo la ukosefu wa maji.Wakaazi wengi wa maeneo hayo hulazimika kununua maji kwa bei ghali na hali hii inaendelea mpaka leo.
Na Devid Geofrey:
Wananchi wa kitongoji cha Bweyaja kijiji cha Omurulama kata ya Chanika wilaya ya Karagwe mkoani Kagera wameiomba serikali ya Rais Dr. Samia Suluhu Hassan iwasaidie maji ili waondokane na kero ya kutumia maji ya madimbwi yanayopatikana baada ya mvua kunyesha.
Wakizungumza kupitia mkutano wa hadhara hivi karibuni mbele ya diwani wa kata hiyo bwana Longino Wilbard aliyeambatana na viongozi mbalimbali kwa lengo la kusikiliza na kutatua kero zao, Wananchi hao wamesema kwa sasa wanalazimika kutumia maji ya madimbwi kwa matumizi ya kupikia na kufua nguo jambo linalohatarisha maisha yao.
Bwana Abdallah Said ni mwenyekiti wa kijiji Omurulama kata ya Chanika amesema licha ya serikali kuahidi kusogeza huduma ya maji kwa wananchi, wakazi wa kitongoji cha Bweyaja kwao maji ni kitendawili ambacho mpaka leo kimekosa mtu wa kukitegua.
Naye mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) kata ya Chanika bw. Peter Paul amesema serikali ya Dr. Samia inasimamia vyema ilani yake hivyo wananchi wawe na subira.
Waswahili wanasema uchungu wa mwana aujuaye mzazi, Bwana Longino Wilbard ni diwani wa kata hiyo, amemshukuru mbunge wa jimbo la Karagwe Innocent Bashungwa chini ya Rais Dr. Samia kwa kuwatengea pesa zitakazotumika kutekeleza miradi ya maji ili kuondoa kero hiyo ifikapo June mwaka 2024.