Karagwe FM
Karagwe FM
1 May 2026, 10:40 am

Mkuu wa wilaya ya Missenyi Kanali mstaafu Hamis Mayamba Maiga. Picha na Resicius John
Mapato ya halmashauri ya wilaya ya Missenyi mkoani Kagera hukusanywa kutokana na vyanzo mbalimbali vya mapato ambapo kwa mujibu wa taarifa ya mkaguzi wa vyama vya ushirika wa wilaya hiyo mauzo ya kahawa mnadani yamechangia zaidi ya shilingi milioni 338.6 kwa msimu wa 2025/2026
Na Respicius John, Missenyi
Katika kikao cha viongozi wa vyama vya ushirika wa Kahawa AMCOS kilichoitishwa na Mkuu wa wilaya Missenyi mkoani Kagera Kanali mstaafu Hamis Mayamba Maiga mkaguzi wa kahawa wilaya ya Missenyi Amon Lugeiyamu amesema kuwa katika msimu wa kahawa wa mwaka 2025/2026 wilaya hiyo imekusanya na kuuza kahawa mnadani kilo 2,543,940 na kuvuka malengo ya ukusanyaji wa kahawa kilo 2,300,000

Kutoka na makusanyo hayo bwana Amon amesema kuwa halmashauri ya wilaya ilipata mapato jumla ya shilingi 338,695,017/= kutokana na ushuru wa asilimia 3 ya bei kwa kilo moja ya kahawa na kwamba kikosi kazi cha kuzuia magendo kilichoundwa na mkuu wa wilaya ya Missenyi kimechangia katika ongezeko hilo la mapato
Pamoja na kusisitiza uendelevu wa kazi ya kudhibiti magendo ya kahawa, mkaguzi huyo amevitaja vyama kumi vya ushirika vilivyoongoza katika makusanyo ya kahawa katika msimu wa 2025/2026 ambapo pia viongozi wa Amcos wameunga mkono hoja ya kuendeleza udhibiti wa magendo na uvunaji wa kahawa mbichi
Kupitia kikao hicho Mkuu wa wilaya ya Missenyi kanali mstaafu Hamisi Mayamba Maiga ametoa wito kwa wananchi kuzingatia ubora wa kahawa katika msimu ujao unaotarajiwa kuanza tarehe 1 mei 2026 huku akiendelea kutoa onyo kwa watu wanaojihusisha na magendo ya kahawa na kwamba kikosi cha kudhibiti magendo kimejipanga kukabiliana nao
Ikumbukwe kuwa bodi ya kahawa Tanzania kupitia tangazo la tarehe 24 April 2026 imetangaza bei elekezi ya kahawa ya shilingi 4,000/= kwa kahawa ghafi aina ya robusta, shilingi 5,100/= kwa kahawa ghafi aina ya robusta ngumu