Sengerema FM

Msonde athibitisha daraja la JPM kuanza kazi April 2025

25 March 2025, 8:58 pm

Picha ni muonekano wa daraja la JPM Kigongo -Busisi ujenzi wake ulipo fikia kwa sasa.Picha na ofsi yamkoa Mwanza

Kwa sasa sehemu ya barabara ya ushoroba wa ziwa Victoria kutoka Sirari mpani mwa Tanzania na Kenya na Mtukula mpakani mwa Tanzania na Uganda imepita eneo la Kigongo Busisi ambapo imeunganishwa kwa kutumia vivuko vikubwa vitatu vya MV Mwanza, MV Misungwi na MV Sengerema.

Na,Elisha Magege

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma (PIC) imetembelea mradi wa ujenzi wa daraja la JP Magufuli (Kigongo-Busisi) lililopo Mkoa wa Mwanza. Daraja hili, linalounganisha mikoa ya Kanda ya Ziwa na nchi jirani, lina urefu wa takriban kilometa 3.2 na linatarajiwa kubadili maisha ya wananchi.

Akizungumza mara baada ya kutembelea na kukagua daraja hilo, Mwenyekiti wa Kamati ya PIC, Mheshimiwa Augustine Vuma, amesema kuwa mradi wa daraja hilo una thamani ya bilioni 610 na umefikia asilimia 97.

Sauti ya Mwenyekiti wa Kamati ya PIC, Mheshimiwa Augustine Vuma akizungumzia mradi wa daraja la Kigingo-Busisi

Aidha, Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Ujenzi Dkt. Charles Msonde amesema daraja la J.P Magufuli (Kigongo Busisi)KM 3 litaanza kutumika rasmi Aprili 30 mwaka huu.

Sauti ya Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Ujenzi Dkt. Charles Msonde akizungumzia kukamilika kwa Daraja la JPM

Kwa upande wake, Meneja wa TANROADS Mkoa wa Mwanza, Mhandisi Ambrose Pascal, amethibitisha kuwa daraja limefika hatua za mwisho na kuwa katikati ya mwezi Aprili 2025, magari yataanza kupita.

Sauti ya Meneja wa TANROADS Mkoa wa Mwanza, Mhandisi Ambrose Pascal akizungumzia hatua zilipo fikia za daraja la JPM

Daraja hilo limejengwa kwa lengo la kuunganisha Barabara Kuu ya Usagara – Sengerema Geita KM90 ambayo ni sehemu ya barabara iliyopo kwenye Ushoroba wa Ziwa Victoria inayoanzia Sirari mpakani mwa Tanzania na Kenya hadi Mutukula mpakani mwa Tanzania na Uganda