Sengerema FM
Sengerema FM
4 March 2025, 8:41 pm

Bibi amfanyia ukatili mjukuu wake kwa kumumwagia chai ya moto sehemu mbalimbali za mwili wake baada ya kuchelewa kurudi nyumbani kutoka sokoni alikokuwa amemuagiza kwenda kuuza sambusa.
Na Emmanuel Twimanye
Mtoto mwenye umri wa miaka 14 katika Mtaa wa Misheni Wilayani Sengerema Mkoani Mwanza amejeruhiwa sehemu mbalimbali za mwili wake baada ya kudaiwa kumwagiwa chai ya moto na bibi yake kwa sababu ya kuchelewa kurudi nyumbani.
Akizungumzia tukio hilo mtoto anaedaiwa kufanyiwa ukatili huo amesema kuwa alikwenda sokoni kuuza sambusa za bibi yake na kuchelewa kurudi nyumbani ndipo alipofanyiwa ukatili huo wa kinyama na bibi yake.
Paulina James ambaye ni bibi anayetuhumiwa kufanya ukatili kwa mtoto huyo amekana kufanya kitendo hicho huku akimtishia mtoto huyo kumfukuza nyumbani kwake.
Baadhi ya wananchi wa mtaa huo wamesikitishwa na tukio hilo na kuiomba serikali kumchukulia hatua kali kisheria bibi huyo ili iwe fundisho kwa watu wengine wenye tabia kama hiyo.
Mwenyekiti wa mtaa wa Misheni Joseph Protas amethibitisha kutokea kwa tukio hilo na kuagiza mtoto huyo kupelekwa Hospitalini kupatiwa huduma ya matibabu kabla ya hatua za kisheria kuchukuliwa dhidi ya Bibi huyo.