Orkonerei FM

“Barabara zitajengwa zimechelewa kwa sababu ya madhara ya mvua”

24 September 2024, 7:12 pm

Mkuu wa Mkoa Wa Manyara Bi. Queen Sendiga akihutubia katika mkutano wa hadhara kijiji cha Terrat wilaya ya Simanjiro leo Septemba 24,2024. (Picha na Evanda Barnaba)

Na Dorcas Charles

Mkuu wa mkoa wa Manyara Queen Sendiga leo tarehe 24 Novemba amefanya ziara ya kukagua miradi ya maendeleo na kusikiliza kero za wananchi katika kijiji cha Terrat kata ya Terrat wilayani Simanjiro, katika ziara yake amekagua kituo cha afya cha Terrati na baadaye kuzungumza na wananchi katika eneo la mikutano kijijini hapa.

Wakati akizungumza na wananchi katika eneo hilo amewaahidi kuhakikisha wodi ya kujifungulia wakina mama itakamilika ili kusaidia afya ya mama na mtoto wakati wa kujifungua, pia kuwasihi wanawake kutumia M-Mama (mpango mkakati wa serikali wakinamama waweze kupata unafuu haraka wakati wa kujifungua.)

Mkuu wa Mkoa Sendiga amewatoa hofu wananchi wa kata ya Terrat kuhusu miundombinu ya barabara kwani serikali tayari imetenga bajeti kwaajili ya kutengeneza miundombinu ya barabara ambayo itawasaidia Wananchi wa Simanjiro katika biashara ya mifugo pamoja na mazao.

Wakati akimalizia mkutano na wananchi wa kata ya Terrat amewataka kubadili mila na tamaduni ambazo zinamkandamiza mwanamke na kuwapa nafasi sawa ya Elimu watoto wakike katika jamii zao.