Karagwe FM

‘Amani Kwanza’ Kagera wahofia video za kashfa dhidi ya Rais Samia

22 September 2024, 6:11 pm

Mwenyekiti wa umoja wa Amani Kwanza Ndugu Maulid Rashidi Kambuga. Picha na Theophilida Felician

Wananchi na makundi mbalimbali ya kutetea haki za binadamu mkoani Kagera wameitaka serikali kuchukua hatua thabiti dhidi ya viashiria vyote vyenye nia ya uvunjifu wa amani vilivyoanza kujitokeza kwa kasi hapa nchini.

Theophilida Felician

Katika kusherehekea siku ya amani duniani inayoashimishwa kila  tarehe 21 septemba ya  kila mwaka   wito umetolewa kwa umma mkoani Kagera na nchi kwa ujumla kuungana pamoja na kuendelea  kuitunza na kudumisha amani  iliyodumu kwa muda mrefu  huku serikali ikisisitizwa  kuchukua hatua za haraka  kivishughulikia na kuvidhibiti viashiria vya uvunjifu wa amani vinavyojitoleza kwa kasi maeneo mbalimbali nchini.

Yameelezwa hayo na wananchi pamoja na taasisi ya umoja wa Amani Kwanza wakati wakihojiwa na Redio Karagwe Manispaa ya Bukoba mkoani Kagera ambapo awali mwenyekiti wa umoja wa Amani Kwanza Ndugu Maulid Rashidi Kambuga amesema kuwa kwa sasa kumekuwepo na masuala yenye kubeba viashiria vya uvunjifu wa amani kupitia nyanja mbalimbali akitolea mfano wa vidio chafu zenye jumbe za kichochezi zinazosambazwa mitandaoni na kuwafikia wananchi zikimtaja kiongozi mkuu wa nchi Rais Dkt Samia Suluhu Hassan kuwa ni muuaji jambo ambalo ni hatari sana kwa amani ya nchi.

Amesema kama jitihada za haraka hazitofanyika na kuyadhibiti haya kwa kuwabaini wahusika ili kuchukuliwa hatua kwa mujibu wa sheria yaweza tokea yasio mazuri tunakoelekea maana baadhi ya watu wasioitakia mema Tanzania wako macho hawajalala ndiyo maana chokochoko za hapa na pale zinaanza kupenyapenya ili kuhakikisha wanaididimiza amani iliyotukuka na kudumu kwa kipindi kirefu tangu kupata uhuru.

Sauti ya mwenyekiti wa umoja wa amani kwanza Ndugu Maulid Rashidi Kambuga
Mmoja wa wajumbe wa Jumuiya ya Amani Kwanza mzee Benard Pastory . Picha na Theophilida Felician

Kwa upande wao wananchi akiwemo Benard Pastory amesema kuwa ili amani kudumu ni vyema kila mmoja kuanzia ngazi ya chini hadi juu kulizingatia ipasavyo suala la maadili ambalo linaunganisha vitu vyote vyenye misingi imara kwa kila mtu na kwa kufanya hivyo suala la amani halitachezewa kama baadhi ya watu wanavyodhani ambapo pia Liston Kikanja ameeleza kwamba taifa letu lina amani tofauti na ilivyo kwa mataifa mengine yanayotaabika kwa sasa baada ya kukosekana kwa amani .

Benard Pastory na Liston Kikanja

Hata hivyo Adolf Alane amevitaja baadhi ya vitu ambavyo kama havitotizamwa na kushughulikiwa vyaweza hatarisha amani ni pamoja na wimbi la rushwa katika siasa huku Hamza Idd akifafanua kuwa wananchi hawako tayari kuona amani inadondoshwa.

Adolf Alan na Hamza Idd

Kila mwaka ifikapo tarehe 21 Septemba ni siku ya amani duniani.