Zenj FM
Zenj FM
06/04/2026, 15:16

Mbunge wa Jimbo la Fuoni, Asha Hussein Saleh amesema mashindano hayo yanakusudia kuenzi mchango wa Karume katika Mapinduzi ya Zanzibar na Muungano. Pia ameahidi kuendeleza michezo ya asili ili kurejesha umaarufu wake katika jamii.
Na Mary Julius
Mbunge wa Jimbo la Fuoni, Asha Hussein Saleh, amezindua rasmi mashindano ya michezo ya bao na drafti, ikiwa ni sehemu ya kumuenzi muasisi wa Mapinduzi ya Zanzibar, hayati Abeid Amani Karume.
Uzinduzi huo umefanyika katika eneo la Fuoni Kiembeni, ukihusisha washiriki kutoka Tanzania Bara na Zanzibar, ambapo michezo hiyo ilielezwa kuwa ni miongoni mwa burudani alizozipenda sana hayati Karume.
Akizungumza baada ya uzinduzi huo, Mbunge Asha Hussein Saleh amesema lengo la mashindano hayo ni kuenzi mchango wa kiongozi huyo, hususan katika kuasisi Mapinduzi ya Zanzibar pamoja na Muungano wa Tanganyika na Zanzibar.
Aidha, mbunge huyo ameahidi kuendeleza na kuhamasisha michezo ya asili kama bao na drafti, ambayo kwa sasa inaonekana kupoteza umaarufu katika baadhi ya maeneo ya Zanzibar, ikiwemo Jimbo la Fuoni

.Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Mchezo wa Drafti Tanzania, Salum Simba, amesema mashindano hayo yaliyowashirikisha wachezaji 37 yatasaidia kuimarisha mshikamano na uhusiano mwema kati ya wananchi wa Zanzibar na Tanzania Bara.
Naye Mratibu wa mashindano hayo, Mohamed Abdallah Salum, ameeleza kuwa michezo hiyo inaendeshwa kwa mfumo wa makundi nane, ili kuhakikisha ushindani wa haki na wa kuvutia kwa washiriki wote.
Baadhi ya washiriki wa mashindano hayo wameeleza matumaini yao ya kufanya vizuri na kuibuka washindi, huku wakiahidi kutoa ushindani mkali katika kila hatua ya mashindano.
Zawadi mbalimbali zitatolewa kwa washindi ikiwemo pesa taslimu na kikombe kwa mshindi wa kwanza, wapili na watatu.