Zenj FM
Zenj FM
4 February 2026, 10:54 pm

Na Mary Julius.
Mkurugenzi wa Tiba wa Wizara ya Afya Zanzibar, Dkt. Msafiri Marijani, amewataka wananchi kujitokeza kwa wingi katika kambi za matibabu ya bure ili kupima afya zao, hatua itakayosaidia kugundua mapema maradhi yasiyoambukiza na kupunguza athari zake kwa jamii na taifa kwa ujumla.
Dkt. Marijani ametoa wito huo wakati wa ufunguzi wa kambi ya siku nne ya upimaji wa afya, iliyoandaliwa kwa ushirikiano kati ya Hospitali ya Taifa Muhimbili, Wizara ya Afya Zanzibar na Vodacom Tanzania Foundation.
Amesema kambi hizo ni sehemu ya mkakati wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar wa kusogeza huduma za afya karibu na wananchi, kwa lengo la kuwafikia watu wengi zaidi na kuwaondolea vikwazo vya kifedha vinavyowakwamisha kupata huduma za matibabu.
Amebainisha kuwa kwa sasa dunia inashuhudia ongezeko kubwa la maradhi yasiyoambukiza, huku magonjwa ya moyo yakiongoza kwa kusababisha vifo, yakifuatiwa na ugonjwa wa kisukari, hali ambayo imekuwa mzigo mkubwa kwa familia na serikali.
Kwa mujibu wa Dkt. Marijani, kambi hiyo ya siku nne inalenga pia kuwajengea wananchi utamaduni wa kupima afya mara kwa mara, ili kuzuia madhara makubwa yanayotokana na maradhi yasiyoambukiza ambayo mara nyingi hugundulika yakiwa katika hatua za mwisho.
Kwa upande wake, Daktari Bingwa wa Upasuaji wa Hospitali ya Taifa Muhimbili, Dkt. Juliet Magandi, amesema kambi hiyo inafanyika kwa ushirikiano wa karibu kati ya Hospitali ya Muhimbili, Wizara ya Afya Zanzibar na Kampuni ya Vodacom Tanzania.
Dkt. Magandi amesema wamejipanga kuwafikia wananchi zaidi ya elfu sita kwa kutoa huduma za kibingwa bila malipo, akiongeza kuwa Hospitali ya Taifa Muhimbili ina zaidi ya miaka 120 tangu kuanzishwa kwake na ina madaktari bingwa wa fani mbalimbali.
Amesema kambi hiyo inalenga pia kujengeana uwezo kati ya madaktari wa Muhimbili na wale wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, huku lengo kuu likiwa ni kugundua mapema maradhi yasiyoambukiza ambayo mara nyingi hayana dalili za awali.
Naye Meneja wa Vodacom Tanzania Foundation, Sandra Oswald, amesema lengo la ushirikiano huo ni kuwapatia Wazanzibari huduma za kitabibu za kibingwa, hususan zinazohusiana na maradhi yasiyoambukiza.
Ameeleza kuwa zaidi ya asilimia 30 ya vifo husababishwa na maradhi yasiyoambukiza, na kusisitiza kuwa Vodacom inalenga kuwawezesha wananchi kiafya ili waweze kushiriki kikamilifu katika shughuli za maendeleo.
Kwa upande wao, wananchi waliopata huduma wamepongeza zoezi hilo na kuomba liendelezwe zaidi. Zuhura Khamis Nassor amesema amepata vipimo na kukutana na madaktari bingwa, huku akiomba kambi hizo zipelekwe hadi vijijini na mashambani.
Naye Abdalla Pandu amesema kambi hiyo imemsaidia kufahamu hali ya afya yake na kupata matibabu, amezihimiza taasisi na makampuni mengine kuiga mfano wa Vodacom Tanzania.
Kambi hiyo ya siku nne imeanza siku ya Jumanne na inatarajiwa kumalizika siku ya Ijumaa, tarehe 6 mwezi wa pili.