Zenj FM
Zenj FM
20 July 2025, 5:36 pm

Mkurugenzi wa Baraza la Mji Kati, Dkt. Mwanaisha Ali Said,amewahimiza wananchi kubadilika kifikra na kuchukulia usafi kama jukumu la pamoja kwa ajili ya afya na maendeleo ya jamii.
Wananchi wa Wilaya ya Kati wametakiwa kuzingatia suala la usafi wa mazingira katika maeneo yao kwa kuendeleza tabia ya kusafisha mazingira yao wenyewe, badala ya kusubiri kusafishiwa na serikali kama ilivyozoeleka.
Dkt. Mwanaisha ametoa kauli hiyo mara baada ya kushiriki katika zoezi la usafi lililofanyika katika barabara ya Mwera-Pongwe hadi kwa Kozi, Wilaya ya Kati.
Dkt. Mwanaisha amesema suala la usafi linapaswa kuwa endelevu na la kila mwananchi, na si jambo la kusubiri kuhamasishwa au kufanyiwa na mamlaka husika.
Kwa upande wake, Afisa Uhusiano wa Baraza hilo, Fatma Ali Said, amesema zoezi hilo la usafi lililoshirikisha watendaji wa Baraza na wananchi wa Mwera Pongwe lilikuwa na lengo la kuhamasisha jamii kuhusu umuhimu wa kufanya usafi wa mara kwa mara, ili Wilaya hiyo ibaki safi na salama kwa afya ya wakazi wake.
Nao baadhi ya wananchi walioshiriki katika zoezi hilo, wakiwa wawakilishi wa wenzao, wameahidi kuendeleza juhudi hizo kwa kuendelea kufanya usafi na kuwaelimisha wenzao umuhimu wa kulinda mazingira kwa maslahi yao na ya vizazi vijavyo.
Zoezi hilo la usafi lilifanyika kuanzia eneo la Bago la Mkoa hadi Koani kwa kutumia mbinu mbalimbali za usafi na kushirikisha nguvu kazi kutoka kwa watendaji wa Baraza la Mji Kati pamoja na wananchi wa maeneo husika.