Zenj FM
Zenj FM
9 May 2025, 4:41 pm

“Uchunguzi wa mapema uliwasaidia kupata tiba kwa wakati, hali iliyowezesha matibabu kuwa na ufanisi mkubwa na hatimaye kupona kabisa saratani ya matiti“
Na Mary Julius
Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Saratani Zanzibar Dk Hellen Makwani ametoa wito kwa jamii, hasa wanaume, kujenga utamaduni wa kupima afya mara kwa mara, hususan kwa ajili ya uchunguzi wa tezi dume — aina ya saratani inayoongoza kwa kusababisha vifo kwa wanaume nchini.
Dk Hellen ametoa kauli hiyo katika mafunzo maalum yaliyotolewa kwa waandishi wa habari, yaliyoandaliwa na wizara ya afya Zanzibar yaliyofanyika katika hoteli ya Golden Tulip uwanja wa ndege wa Zanzibar, ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya Wiki ya Afya Zanzibar.
Hellen amesema moja ya njia muhimu za kukabiliana na kuenea kwa magonjwa ya saratani visiwani Zanzibar ni kwa jamii kubadili mtazamo na tabia kuhusu afya, hasa kwa kuhakikisha wanajitokeza kufanya uchunguzi wa afya mara kwa mara.
Wakizungumza katika mafunzo maalum ya kuhamasisha mapambano dhidi ya maradhi yasiyoambukiza NCD’s visiwani Zanzibar, mahanga wa ugonjwa wa saratani ya matiti wamesema kufanya vipimo mapema kumechangia katika mafanikio ya matibabu yao.
Aidha wamesema uchunguzi wa mapema uliwasaidia kupata tiba kwa wakati, hali iliyowezesha matibabu kuwa na ufanisi mkubwa na hatimaye kupona kabisa saratani ya matiti.