Zenj FM

Bei ndogo ya mwani kilio kwa wakulima Pwani Mchangani

25 September 2024, 4:22 pm

zao la Mwani. Picha na Mary Julius

Na Mwanaisha Msuko.

Wananchi wa Pwani Mchangani Mkoa wa Kaskazini, wilaya ya Kaskazini A Unguja wameiomba serikali kuongeza bei ya mwani ili kuweza kumkomboa mkulima wa zao hilo.

Wakizungumza na Zenji FM wakulima hao wamesema bei ndogo ya mwani inarudisha nyuma juhudi za wakulima wa mwani kwani wamekuwa wakitumia nguvu kubwa kulima zao hilo ambalo faida yake imekuwa ndogo na haikidhi mahitaji yao.

Aidha wameiomba serikali kuwapatia vifaa ikiwemo kamba, vijiti, taitai, boti na mashine za kusanifu bidhaa hiyo ili iweze kuwasaidia katika kuongeza uzalishaji wa zao hilo lenye faida nyingi kwa bianadamu.

Sauti ya wananchi wa Pwani Mchangani.

Zenj FM haikuishia hapo ilifika hadi katika Idara ya Uvuvi na Mazao ya Bahari na kukutana na Mkurugenzi wa Idara hiyo Salum Sudi Hemedi ambaye amesema serikali inafanya juhudi mbalimbali katika kuhakikisha zao hilo linaongezewa thamani ili kuweza kuwanufaisha wananchi.

Aidha amesema serikali imeshapeleka baadhi ya vifaaa kama kamba, taitai, boti na mashine za kusanifu katika vijiji tofauti ambavyo vinajishughulisha na upandaji wa zao hilo la mwani.