Radio Jamii Kilosa

Kilosa yazindua wiki ya unyonyeshaji Duniani

1 August 2026, 10:45

Wakinamama wanaonyonyesha wakiwa katika uzinduzi wa wiki ya unyonyeshaji duniani yalifanyika zahanati ya Rudewa. Picha na Kadewele Said

Wiki ya Unyonyeshaji Duniani huadhimishwa kila mwaka kuanzia Agosti 1 hadi 7, ikiwa na lengo la kuhamasisha jamii kuhusu umuhimu wa unyonyeshaji wa maziwa ya mama katika kuhakikisha watoto wanapata afya bora, lishe sahihi na ukuaji unaofaa.

Na Asha Madohola

Halmashauri ya Wilaya ya Kilosa imezindua maadhimisho ya Wiki ya Unyonyeshaji Duniani katika Zahanati ya Rudewa, Kata ya Rudewa, kwa lengo la kutoa elimu kwa jamii kuhusu umuhimu wa maziwa ya mama na unyonyeshaji sahihi wa watoto.

Afisa Lishe wilaya ya Kilosa Elisha Kingu

Akizungumza katika uzinduzi huo, Afisa Lishe wa Halmashauri ya Wilaya ya Kilosa, Elisha Kingu, amesema jamii imepewa elimu kuhusu namna sahihi ya kumnyonyesha mtoto, kumshika wakati wa kunyonyesha na kutambua iwapo mtoto anapata maziwa ya kutosha na alisema elimu hiyo itaendelea kutolewa kuanzia Agosti 1 hadi 7, 2026, kupitia vituo vya afya na vyombo vya habari, kwa lengo la kuhakikisha watoto wanapata maziwa ya mama pekee katika miezi sita ya mwanzo na kupunguza changamoto za utapiamlo.

Sauti ya Afisa Lishe wilaya ya Kilosa Elisha Kingu akizungumza
Mgeni rasmi Sabina Sugwa ambaye ni Afisa Tarafa ya Kimamba

Kwa upande wake, Afisa Tarafa wa Kimamba, Sabina Lucas Sugwa, aliyemwakilisha Mkuu wa Wilaya ya Kilosa, amewataka akina mama kutimiza wajibu wa kuwanyonyesha watoto wao na kuwataka wataalamu wa afya pamoja na viongozi kuendelea kutoa elimu na hamasa kuhusu unyonyeshaji na malezi bora ya watoto.

Sauti ya Mgeni rasmi Sabina akizungumza

Naye Mganga Mfawidhi wa Zahanati ya Rudewa, David Philemon Mkuchu aliushukuru uongozi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kilosa pamoja na wadau kwa kuichagua zahanati hiyo kuwa mwenyeji wa uzinduzi huo, akisema tukio hilo limekuwa chachu kwa watumishi wa afya na wananchi wa Rudewa katika kuongeza uelewa kuhusu umuhimu wa unyonyeshaji.

Sauti ya Mganga Mfawidhi Dkt Mkuchu
Wakinamama wanaonyonyesha wakiwa katika ushindani wa kunyonyesha mtoto vizuri

Akizungumza kwa niaba ya akina mama walioshiriki uzinduzi huo, Raheli Lazaro kutoka Rudewa, alisema amefurahishwa na elimu aliyopata, ikiwemo namna sahihi ya kumnyonyesha mtoto, lishe inayofaa kwa mama anayenyonyesha na umuhimu wa mtoto kupata maziwa ya mama pekee katika miezi sita ya mwanzo pia elimu hiyo imewasaidia kufahamu umuhimu wa wazazi kushirikiana katika malezi na kuhakikisha watoto wanapata uangalizi, upendo na malezi bora tangu wakiwa wadogo.

Sauti ya mama anayenyonyesha Rahel Lazaro akizungumza
Afisa Lishe Jackson Kalibwani akimpima mtoto hali ya lishe katika uzinduzi wa Wiki ya Unyonyeshaji Duniani