Radio Jamii Kilosa
Radio Jamii Kilosa
20 May 2026, 15:02

Watoto wa Day Care wanahitaji malezi bora, mazingira salama na elimu ya awali ili kuwajengea msingi mzuri wa maisha yao ya baadaye.
Na Aloycia Mhina
Wamiliki na walezi wa vituo vya kulelea watoto wadogo (Day Care) katika Kata ya Dumila wilayani Kilosa wametakiwa kubadilika katika namna ya utoaji wa malezi kwa watoto ili kwenda sambamba na mabadiliko ya dunia ya sasa yanayohitaji malezi bora na yenye kuzingatia maendeleo ya mtoto.

Wito huo ulitolewa na Afisa Ustawi wa Jamii wa Halmashauri ya Wilaya ya Kilosa, Silivesta Katikaza wakati akifungua mafunzo ya siku 15 kwa wamiliki na walezi wa vituo 20 vya kulelea watoto wadogo katika Kata ya Dumila.
Akizungumza katika mafunzo hayo, Katikaza alisema vituo vya kulelea watoto vina nafasi kubwa katika malezi ya awali na maendeleo ya mtoto, hivyo ni muhimu kwa wamiliki na walezi kuendana na mabadiliko ya sera na sheria za mtoto.
Aidha alisema kuwa hata sera ya mtoto ya mwaka 2008 ilifanyiwa maboresho na kupelekea kutungwa kwa Sheria ya Mtoto ya mwaka 2009 ambayo baadaye nayo iliboreshwa, jambo linaloonyesha umuhimu wa kuendelea kujifunza na kubadilika kulingana na mahitaji ya wakati.

Kwa upande wake, Mratibu wa Mradi wa Kinara, Prisca Norbert alisema kuwa mafunzo hayo yanalenga kuwapa elimu wamiliki na walezi wa vituo vya Day Care kuhusu usajili wa vituo vyao pamoja na mbinu za kujikwamua kiuchumi kupitia miradi na vikoba.

Nao baadhi ya washiriki wa mafunzo hayo akiwemo Monika Gidioni na Saferini Makilila waliwashukuru waandaaji wa mafunzo hayo wakisema yatawasaidia kuboresha malezi ya watoto na kuinua hali zao kiuchumi.
Mafunzo hayo yanadhaminiwa na Taasisi ya Kinara kupitia mdau wa Swisscontact kutoka Morogoro kwa lengo la kuwajengea uwezo kuhusu malezi ya watoto, usajili wa vituo pamoja na shughuli za maendeleo zitakazowaongezea kipato.