Zenj FM

SMZ yaongeza nguvu kukuza lugha ya alama Zanzibar

19 November 2025, 5:41 pm

Katibu wa Baraza la Watu Wenye Ulemavu Zanzibar, Ussi Khamisi Debe,( aliye vaa koti jeusi) akiwa na Makamu Mwenyekiti wa SHIJUWAZA, Ali Omar Makame C kushoto kwake) pamoja na viongozi mbali mbali wa JUWALAZA katika maadhimisho ya siku ya wakalimani Mkoa wa Kasakzini Unguja.

Na Mary Julius.

Serikali ya Mapinduzi Zanzibar imesisitiza dhamira yake ya kuimarisha utoaji wa huduma jumuishi kwa watu wenye ulemavu, hususan katika kukuza na kusambaza matumizi ya lugha ya alama kwenye sekta mbalimbali.

Akizungumza katika maadhimisho ya Siku ya Wakalimani wa Lugha ya Alama Zanzibar yaliyofanyika Chuo cha Mafunzo ya Amali Mkokotoni, Katibu wa Baraza la Watu Wenye Ulemavu Zanzibar, Ussi Khamisi Debe, amesema Serikali inaendelea kuweka mikakati madhubuti kuhakikisha kila taasisi inayotoa huduma kwa jamii inakuwa na uwezo wa kutumia lugha ya alama.

Amesema tayari sekta ya afya imeanza utekelezaji wa mpango wa kuhakikisha kila kituo cha afya kinakuwa na mkalimani wa lugha ya alama, huku sekta ya elimu ikisonga mbele na mpango wa kuyapatia skuli madarasa maalum ya kufundisha lugha hiyo, sambamba na kuwahamasisha wazazi kujifunza ili kuimarisha mawasiliano na watoto wenye ulemavu.

Sauti ya Katibu wa Baraza la Watu Wenye Ulemavu Zanzibar, Ussi Khamisi.

Kwa upande wake  Makamu Mwenyekiti wa SHIJUWAZA, Ali Omar Makame, amesisitiza umuhimu wa kuongeza idadi ya wakalimani wa lugha ya alama nchini.

Makamo mwenyekiti Ametoa mfano wa kipindi cha uchaguzi ambapo Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC) ilihitaji wakalimani katika kila kituo, lakini mpango huo haukutekelezeka kutokana na uhaba wa wataalamu hao.

Ameiomba Serikali kuweka silabasi rasmi ya kufundisha lugha ya alama katika skuli na vyuo, pamoja na kuanzisha bodi maalum ya kusimamia mafunzo na viwango vya ukalimani.

Sauti ya Makamu Mwenyekiti wa SHIJUWAZA, Ali Omar Makame.

Naye Mkurugenzi wa Jumuiya ya Wakalimani wa Lugha ya Alama Zanzibar (JUWALAZA), Kheri Mohammed Simai, amesema maadhimisho ya mwaka huu yamefanyika Kaskazini ili kuongeza uelewa katika maeneo ambayo bado yanahitaji mwamko.

Sauti ya Mkurugenzi wa Jumuiya ya Wakalimani wa Lugha ya Alama Zanzibar (JUWALAZA)

Kwa upande wa jamii ya watu wenye ulemavu, Mwenyekiti wa Jumuiya ya Watu Wenye Ulemavu Mkoa wa Kaskazini Unguja, Haji Khamisi Nyange, amesema mkoa huo umeanza kupata madarasa ya lugha ya alama, lakini bado unahitaji fursa zaidi ili kuongeza idadi ya wataalamu.

Aidha, ameiomba Serikali kuwachukulia hatua wazazi wanaowaficha watoto wenye ulemavu na kuwanyima haki ya kupata elimu.

Sauti ya Mwenyekiti wa Jumuiya ya Watu Wenye Ulemavu Mkoa wa Kaskazini Unguja.