Zenj FM
Zenj FM
2 October 2025, 10:24 pm

Na Mary Julius.
Mgombea urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Chama cha United Democratic Party (UDP), Saumu Rashid, amesema akipata ridhaa ya kuwa rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania atahakikisha kuwa kilimo cha karafuu kinakuwa chanzo kikuu cha maendeleo kwa wananchi wa Zanzibar.
Akizungumza katika mkutano wa kampeni uliofanyika kwenye viwanja vya Magirisi, Wilaya ya Magharibi B, Saumu amesema chama hicho kimejipanga kuhakikisha soko la uhakika kwa karafuu linakuwepo sambamba na kujenga viwanda vikubwa vya kuchakata zao hilo kwa ajili ya soko la kimataifa.
Amesema UDP imelenga kuleta kilimo chenye tija kwa kuwekeza katika zana bora, mbegu bora na utoaji wa mikopo nafuu ili kuwainua wakulima kiuchumi.
Aidha, amesema UDP inatambua umuhimu wa kudumisha Muungano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, akisisitiza kuwa chama hicho kitaweka misingi imara ya kuimarisha mshikamano wa kitaifa.
Kuhusu mahusiano ya kidiplomasia, amesema chama chake kitaweka mkakati madhubuti ili kuhakikisha Tanzania inanufaika kiuchumi na kiusalama kupitia ushirikiano na mataifa mengine.
Kwa upande wake Mgombea mwenza wa urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Chama cha United Democratic Party (UDP), Juma Khamisi Faki, amesema wamejipanga kunadi sera ,na kuwataka Wazanzibari kujitokeza kwa wingi kupiga kura katika uchaguzi mkuu ujao na kukichagua chama cha UDP kwa ajili ya mabadiliko ya kweli.