Zenj FM

Kongamano la Ekaristi liwe somo kwa demokrasia nchini

17 September 2024, 1:20 pm

Katibu mkuu wa Chama cha Mapinduzi Balozi Dk Emmanuel Nchimbi akimsadia Makamu mwenyekiti wa Chadema Bara TUNDU lissu kupanda katika Jukwaa katika Konngamano la dini uwanja wa Uhuru katikati Katibu Mkuu wa Chadema John Mnyika picha na mpiga picha wetu

Na Mwandishi wetu.

Kengele ya wito wa kudumisha amani , umoja ,maelewano na mapatano imeshapigwa na Kanisa katoliki nchini.

KAZI kubwa iliobaki ni ya viongozi wa vyama vya siasa kutimiza wajibu ili kuliweka pamoja Taifa katika ramani yake ya asili.

Kukutanishwa kwa wanasiasa vigogo toka upande wa utawala na upinzani , kufungue pazia na kupata njia itakayoliweka pamoja Taifa kabla hakujachomoza kiza cha majuto.

Wito huo umewataka pia viongozi wa kijamii, dini,wasomi wanataaluma na mashrika yote huru, wakiwemo wahubiri maendeleo ya umoja na wadau wa amani .

Makamo Mwenyekiti wa Chadema Tundu Lissu, Katibu Mkuu wa CCM Balozi Dk Emmanuel Nchimbi na katibu Muu wa CHADEMA John Mnyika wamekutana na kutazamana ana kwa ana wakiwa kwenye kongamano la tano ka ekaristi takatifu katika uwanja wa taifa wa uhuru jijini Dar es salaam.

Wameitwa,wameitikia wito.Hawakupuuza wito huo bali walisimama mbele ya halaiki ya waumini wenzao . Wamesimama huku wakiwa pamoja ndani ya uwanja wa ibada takatifu na mbele ya Mungu.

Uamuzi huo si mdogo au wa hovyo au labda wa kubahatisha .

Badala yake wamethibitisha kiapo chao katika dhima ya kusimamia ustawi wa maendeleo ya Amani ,Utulivu na Upendo.

Hatua ya kukutanishwa kwao ni wito wa moja kwa moja katika kuonyesha kutiiwa mbele ya jamii inayowatazama wakiwa viongozi na wanaotegemewa na jamii.

Viongozi hao kwa kitendo cha kukutana katika ibada moja ,hakutokani na nguvu au ujanja wao bali ni karama toka kwa Mungu.

Wito huo unawataka kuepusha aina yoyoye ya majanga , dhoruba.

Hakuna neno siasa safi, uongozi bora, maendeleo ya uchumi, ustawi wa demokrasia ,utawala wa sheria au kuenzi haki za binadamu iikiwa amani utapuuzwa na kutoweka.

Mahali popte duniani amani, utulivu na umoja vilipokosekana ,mahali hapo palitawaliwa na shari, uchukivu na mporomoko wa maelewano kulitokea,umwagaji damu, vita,maafa na vifo.

Haijatokea na nchi yoyote duniani ambayo imefuzu jambo lolote ikiwa nchi hiyo ilipoteza haiba ya amani na umoja wake wa kitaifa.

Tanzania iliojenga na kudumisha umoja wake, udugu wa watu wake bila kutumia nguvu na ushawishi wa ukabila ,dini, rangi au ukanda, haipaswi ikubali ipoteze tunu ya mshikamano wake.

Kengele ilipigwa kwenye kongamano la tano na ekaristi takatifu imewajumuisha wanasiasa kwa niaba ya vyama na wafuasi wao.

Viongozi wa vyama vikuu CCM na chadema ,wamesimama bege kwa bega mbele ya viongozi wa dini wametuonyesha njia muafaka.

Kusimama kwao uwe mwanzo wa kuelekea katika maelewano thabiiti na kutuma ujumbe utakaodumisha amani badala ya kutokea vurugu, chuki na hamaki.

Siku zote jazba, chuki, husda na hamaki hazijajenga jambo lolote likaleta manufaa , maslahi ya pamoja na ustawi katika nchi yoyote.

Badala yake vitu hivyo vinadhofika hupoteza uhai na maisha ya watu wasio hatia ,kuvuruga amani , maelewano , maendeleo ya kisekta na kuwarudisha nyuma nchi katika umasikini na migawanyiko.

Amani, umoja na utulivu vikitoweka husalia dhiki, shida,hekaheka ,mikasa na hamkani katika jamii.

Pale masuala yanapowekwa nyuma na kususia ushiriki wa mazumgumzo mezani ili yasipatikane maamuzi sahihi, mapatano na utangamano.

Historia siku zote ni mwalimu mkuu katika dunia .Tanzania bila amani isingefafanya lolote katika harakati za kupigania uhuru wake, ukombozi Kusini mwa Afrika na kuhifadhi wapigania uhuru wa kila pembe ya dunia.

Vyama kadhaa vya wapigania uhuru viliweka makaazi yake katika ardhi ya Tanzania ili viweze kupigania uhuru,kutafuta haki ,usawa na umoja katika nchi zao.

Katika vipindi hivyo vyote Tanzania ikikabiliana na mitikisiko misukosuko ya ndani na nje, shida,vita, furaha na misiba kutokana na Taifa kuwa na umoja, amani na utulivu.

Licha ya kuwepo tabu , dhiki na hata upungufu wa baadhi ya bidhaa muhimu za vyakula lakini watanzania wakibaki wakiwa wamoja katika nyakati zote hatimaye kupata ushindi wakiwa pamoja.

Sauti ilitoa wito toka katika kongamano hilo ni sauti muhimu sana kusikilizwa .Si sauti yenye utani au mzaha bali ni wazi viongozi wa vyama vya siasa wanatakiwa kukutanishwa pamoja mezani kujadili hatma ya nchi.

Haitarajiwi kabisa sauti hiyo ya wito wa kudumisha amani, ikapuuzwa na viongozi wa vyama vya siasa ,badala yake kila mmoja apate utayari wa kusimama pamoja na wenzake kama taifa ili kutoiingiza nchi katika mivutano inayoweza kuzungumzika.

Viongozi wa Dini wameonyesha njia ya kujenga demokrasia na misingi ya utwala bora kwa vyama vya siasa kushindana kwa hoja pamoja na kusimamia kwa vitendo usalama wa raia na Mali zao na kujiepusha na sitafahamu iliyojitokeza na kutia doa historia ya Taifa , tutafika muhimu Uhuru na Kazi