Zenj FM
Zenj FM
26 October 2025, 9:43 pm

“CCM imeandaa ilani yenye kurasa 60 ambayo imedhihirisha dhamira ya chama katika kuwaletea wananchi maendeleo ya kijamii na kiuchumi” – Sufian Khamis Ramadhani
Na Mary Julius.
Viongozi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) katika Jimbo la Amani wamewaomba wananchi kutokufanya makosa katika uchaguzi mkuu wa Oktoba 29, na kuhakikisha wanakichagua chama hicho ili kuendeleza maendeleo yaliyofikiwa.
Akizungumza wakati wa kufunga kampeni katika jimbo hilo, MNEC Sufian Khamis Ramadhani amesema CCM imeandaa ilani yenye kurasa 60 ambayo imedhihirisha dhamira ya chama katika kuwaletea wananchi maendeleo ya kijamii na kiuchumi.
Amesema ilani hiyo imebeba mambo mengi mazuri, na kuwaomba wabunge pamoja na wawakilishi kuhakikisha wanatekeleza kwa vitendo yale yaliyopangwa ili kuwanufaisha wananchi.
Kwa upande wake, Mgombea ubunge wa jimbo la Amani, Abdul Yusuf Maalum amesema endapo wananchi watampa ridhaa ya kuongoza, atahakikisha anasimamia utekelezaji wa kila kilichoainishwa katika ilani ya CCM.
Naye Mgombea wa Uwakilishi wa jimbo hilo Masoud Amour Masoud amesema kampeni zao zimewafikia wananchi nyumba kwa nyumba na kwa makundi mbalimbali yakiwemo bodaboda na mama lishe, na wana imani kubwa ya kushinda katika uchaguzi huo.
Ameahidi kudumisha ushirikiano na Mbunge wa jimbo hilo katika kuwaletea maendeleo wananchi pamoja na kulinda amani.
Katibu Mwenezi wa CCM Jimbo la Amani, Ismail Amer Kipimo, amewapongeza viongozi wakuu wa chama kwa mafanikio yaliyopatikana kupitia utekelezaji wa ilani ya mwaka 2020–2025, hali iliyowarahisishia wagombea kufanya kampeni zenye ufanisi.