Kahama FM
Kahama FM
7 July 2026, 4:36 pm

‘‘Baadhi ya dawa kuharibika kwa muda mfupi, hilo hatuta kubali na badala yake pokeeni dawa zenye muda wake juu ya miezi 12’’
Halmashauri zote za mkoa wa Shinyanga zimeagizwa kutokupokea dawa za matumizi ya binadamu zenye muda wa matumizi uliobaki chini ya miezi 12 ili kulinda matumizi mabaya ya fedha za serikali.
Agizo hilo limetolewa na mkuu wa mkoa wa Shinyanga Mboni Mhita, wakati wa baraza maalum la kupitia taarifa ya mdhibiti na mkaguazi mkuu wa hesabau za serikali (CAG) katika halmashauri la Ushetu wilayani Kahama mkoani Shinyanga.

Aidha, Mhita amesema kuwa kwa sasa halmashauri zote 6 za mkoa huo, zinapaswa kuweka utaratibu mzuri, ambao utasaidia kuondokana na changamoto hiyo ya kuwa na dawa ambazo muda mfupi zinaisha matumizi yake.

Awali, Kaimu afisa mipango wa halmashauri ya Ushetu Charles Machuba, akiwasilisha taarifa ya hoja za CAG, majibu ya menejimenti na hali utekelezaji wa mapendekezo ya ukaguzi kwa mwaka wa fedha 2025/2026, amesema mkaguzi alitoa mapendekezo kwa menejimenti kuweka utaratibu wa kutambua na kuondoa kwa wakati dawa zilizokaribia kuharibika na kuisha muda wa matumizi.

Kwa upande wao Mkurugenzi wa halmashauri hiyo Khadija Kabojela na mwenyekiti wa halmashauri hiyo ya Ushetu Gagi Lala, wamesema kuwa wapokea maagizo hiyo na watayatekeleza ili kuondokana na changamoto hiyo ya dawa kuisha muda wake mapema.
