Kahama FM
Kahama FM
28 June 2026, 3:06 pm

Wajasiliamali katika kata ya Nyahanga Halmashauri ya Manispaa ya Kahama mkoani Shinyanga, wametakiwa kuchangamkia fursa za mikopo ya asilimia 7% na 10% yenye masharti nafuu ili kujikwamua kiuchumi na kuongeza vipato vyao.
Zaidi ya wajasiliamali 74 wa kata ya Nyahanga wamepatiwa mafunzo ya siku 5 ya ujalimali bure, huku yakilenga kuwapatia njia bora ya utengenezaji wa Batic na bidhaa za usafi, vipodozi, kilimo biashara na masoko.

Kauli hiyo imetolewa leo na diwani wa kata ya Nyahanga Josephina Kilimba, wakati wa kufunga mafunzo hayo ya siku tano kwa wajasiliamali mbalimbali wa kata hiyo, ambapo mafunzo yalikuwa ni bure kwa wajasiliamali, aliyotolewa na Taasisi ya Star Enterpreneur General kwa kushirikiana na diwani Kilimba.
Aidha, Kilimba amesema baada ya kupatiwa mafunzo hayo wanapaswa wajasiliamali hao kupata mitaji kwa ajili ya kufanya biashara kwa kupata mikopo ya 7% na 10% inayotolewa na serikali, na kuwataka kushirikiana na maafisa maendeleo kupata mikopo hiyo, huku akiwaahidi kuwapatia eneo la shamba darasa.

Awali, akisoma risala kwa mgeni rasmi Neema Joseph amesema kuwa wamejifunza mambo mbalimbali yatakayowasaidia katika shughuli zao za kiuchumi, huku wakiiomba kupatiwa mikopo nafuu pamoja na ruzuku kwa vifaa vya ujasilimali.

Kwa upande wake, katibu wa wajasiliamali wilaya ya Kahama Devother Herry, amewataka wajasilimali hao kuwa na kitambulisho cha Mjasiliamali ili kuweza kupata fursa mbalimbali ikiwemo mikopo ya 7%, huku Afisa maendeleo kata ya Nyahanga Agnes Mahewa akisema kuwa kabla ya kupata mkopo wanapaswa kupata kwanza elimu ya biashara.

Naye mkurugenzi wa Taasisi ya Star Enterpreneur General Danfod Kusaga, amesema kuwa kabla ya kuwa mjasiliamali wanapaswa kwanza kujifunza na kupata mafunzo mbalimbali ili kuweza kufanya shughuli za kiuchumi kwa kuwa na uhakika na wanachokifanya.
