Kahama FM

KAHAMA:Washinda Kaburini wakimuomba Rais Samia awasaidie kurejesha Ardhi yao iliyochukulkiwa na CCM.

November 9, 2022, 12:32 pm

Wajukuu wa Marehemu Mussa Sekke Wakiwa Wamekaa kwenye Kaburi 

Katika hali isiyo ya kawaida wajukuu wa Marehemu Musa Sekke Kasuka wa kijiji cha Mpera Kata Ya Isagehe wilayani Kahama mkoani Shinyanga wameamua kushinda kwenye kaburi la babu yao Wakimuomba Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan kuwasaidia kupata eneo lilioachwa na babu yao ambalo limechukuliwa na Chama cha Mapinduzi (CCM).

Wajukuu hao wakiongozwa na Mussa Makoye na Edward makoye wamesema kuwa wamefatilia eneo hilo kwa muda wa ishirini tangu mama yao alipokuwa hai lakini wameshindwa kurejeshewa eneo hilo licha ya kufuata taratibu zote za Kisheria ngazi ya Kijiji.

Akiongea na Kahama Fm Edward Makoye amesema kuwa Eneo hilo lina Miti ya miembe na Misonobari ambayo ilipandwa na babu yao pamoja na nyumba moja chakavu aliyokuwa anaishi babu yao na katika eneo hilo kuna kaburi ambalo walimzika babu yao.

.

Naye Mussa makoye ameongeza kuwa familia yao iliwakatia eneo lingine serikali ya kijiji cha Mpera ili wajenge Ofisi ya Kijiji chini ya Diwani aliyekuwa madarakani Andrew Gerado pamoja na mtendaji aliyemtaja kwa jina moja la Clement ila wanashang’aa kwanini wanalitaka eneo lenye kaburi na Nyumba ya Babu yao.

Kwa upande wake Baba mdogo wa wajukuu hao Maige Charles amesema kuwa Eneo hilo la Marehemu babu yao alilipata mwaka 1974 kwenye Operation kijiji na alifariki mwaka 1982 ambapo Chama cha mapinduzi walimuomba mke wa marehemu kutumia nyumba hiyo kama Ofisi na hadi alipofariki.

.

Naye Mzee wa maarufu wa Kijiji cha Mpera Mzee Omari Mayala mwenye miaka (102) amesema kuwa yeye na Marehemu Mzee Mussa seke walipakana mipaka ya viwanja vyao  na mashamba hayo yalikuwa ni ya ujamaa na waliyapata kwenye Operetion kijiji mwaka 1974.

.

Akiongea kwa njia ya simu Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi Wilaya ya Kahama Thomas Mnyonga amesema hajapata taarifa rasmi za swala hilo japo anazisikia chinichini na kwamba mali zote za chama zipo chini ya Baraza la wadhamini la chama na amewashauri wajukuu wa Mzee Sekke kufata taratibu za kisheria ili haki iweze kutendeka kwa kila mmoja kuliko kushinda Kaburini.

.