Kibanda:Tumejipanga kuhakikisha kila raia anasherehekea kwa usalama krismasi na mwaka mpya
12 December 2023, 16:48
Jeshi la polisi wilayani Kyela limewataka wananchi wote kusherehekea sikukuu za krismasi na mwaka mpya kwa utulivu na amani.
Na James Mwakyembe
Kuelekea sikukuu za mwisho wa mwaka krimasi na mwaka mpya Jeshi la Polisi wilayani Kyela limewataka wananchi wote wilayani hapa kuhakikisha wanasherehekea kwa utulivu mkubwa ili kujikinga na majanga yanayoweza kuwapata.
Hayo yamesemwa na SSP Lwitiko Kibanda wakati akizungumzia mikakati ya jeshi la polisi wilayani hapa kuelekea sikukuu za mwisho wa mwaka ambapo amesema jeshi hilo limejipanga kuhakikisha kila raia anasherehekea sikukuuu hizi za mwisho wa mwaka kwa usalama pasina majanga yoyote.
Pia mkuu huyo wa polisi wilaya ya Kyela amepiga marufuku disko toto na kuwataka wamiliki wa kumbi za starehe kuhakikisha ifikapo saa 12 jino watoto wote katika kumbi hizo hawawi ndani ya kumbi hizo za muziki.
Kuhusu vyombo vya moto SSP Kibanda amewataka waendesha Pikipiki maarufu kama bodaboda,madereva wa magari pamoja na waendesha pawatila kufuata na kuzingatia suala la usalama barabarani pindi watumiapo vyombo vyao.
Kuhusu oparasheni ASP Kibanda amesema mpaka sasa jeshi hilo linaendelea na misako ambapo ametumia muda huo kuwashukuru wananchi wilayani hapa kwa ushirikiano wanaoutoa kwa jeshi hilo pale panapotokea kadhia mbalimbali miongoni mwao
Amehitimisha kwa kuwatakia wananchi wote wilayani hapa sikukuu njema na kuwataka kusherehekea kwa utulivu na kujiepusha na vitu vinavyoweza kuvunja amani wakati wote wa sikukuu za krismasi na mwaka mpya.