Pambazuko FM Radio
Pambazuko FM Radio
18 November 2025, 7:14 pm

Picha ya jengo la afya linalojengwa Hospitali ya Halmashauri ya Mlimba. Picha na Kuruthum Mkata
Nimeridhishwa na jitihada mnazofanya katika kuboresha huduma za afya; miradi inaendelea kwa kasi na kwa ubora unaotakiwa,” alisema Profesa Tumain Nagu.Naibu katibu mkuu Wizara ya Tamisemi anayeshughulikia Afya.
Na Elias Maganga
Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) anayeshughulikia masuala ya afya, Profesa Tumain Nagu, tarehe 17 Novemba mwaka huu, amefanya ziara ya kukagua miradi ya afya katika Halmashauri ya Wilaya ya Mlimba.
Katika ziara hiyo, Profesa Nagu alitembelea na kukagua miradi mbalimbali ikiwemo jengo la upasuaji, wodi ya wazazi, wodi ya watoto, nyumba za watumishi pamoja na jengo la utawala.
Baada ya ukaguzi huo, amesema ameridhishwa na kasi na ubora wa utekelezaji wa miradi hiyo pamoja na namna huduma za afya zinavyotolewa katika halmashauri hiyo.

Pamoja na pongezi hizo, Naibu Katibu Mkuu alitoa maagizo kwa uongozi wa halmashauri ikiwemo kuhakikisha watumishi wanaodai stahiki zao wanalipwa mara moja, na kuboresha usalama wa miundombinu kwa kufunga grili kwenye milango pamoja na kamera za ulinzi (CCTV).

Akitoa taarifa ya hospitali, Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Wilaya ya Mlimba, Dkt. Willy Kopela, alimweleza Naibu Katibu Mkuu changamoto zinazoikabili hospitali hiyo ikiwemo upungufu wa watumishi na uhaba wa nyumba za watumishi, hali inayochangia ugumu katika utoaji wa huduma bora.

Prof Nagu Amesema Serikali inaendelea kuzifanyia kazi changamoto zote ili wananchi wapate huduma stahiki.
Katika ziara yake hiyo Profesa Nagu aliyoifanya Novemba 17,2025 katika Halmashauri hiyo,pia alitembelea Zahanati ya Mbingu, pamoja na eneo la ujenzi wa Kituo cha Afya Namwawala.