Pambazuko FM Radio
Pambazuko FM Radio
11 March 2026, 8:08 pm

Fedha hizo zimetolewa ili kupunguza changamoto ya uhaba wa vyumba vya madarasa inayoikabili shule hiyo
Na Katalina Liombechi
Kata ya Kibaoni imepokea kiasi cha shilingi milioni 44 kutoka katika fedha za ndani za Halmashauri ya mji wa ifakara kwa ajili ya ujenzi wa vyumba viwili vya madarasa katika Shule ya Sekondari Mabukula, hatua inayolenga kuboresha mazingira ya kujifunzia kwa wanafunzi wa shule hiyo.
Awali Mwalimu Mkuu wa Shule hiyo amesema shule inakabiliwa na upungufu wa vyumba viwili vya madarasa, hali inayosababisha msongamano wa wanafunzi darasani akieleza kuwa ujenzi wa madarasa hayo utasaidia kupunguza changamoto hiyo na kuboresha mazingira ya kujifunzia na kufundishia.
Akizungumza leo Machi 11, 2026 wakati akiungana na wananchi katika zoezi la kujitolea kuchimba msingi tayari kwa kuanza ujenzi wa madarasa hayo, Diwani wa Kata ya Kibaoni, Mheshimiwa Rashid Namtuka, amesema fedha hizo zimetolewa ili kupunguza changamoto ya uhaba wa vyumba vya madarasa inayokabili shule hiyo.
Mheshimiwa Namtuka amewapongeza wananchi kwa kujitokeza kwa wingi kushiriki shughuli za maendeleo na kusisitiza kuwa ushirikiano kati ya serikali na wananchi ni nguzo muhimu katika kufanikisha miradi ya maendeleo katika jamii.

Wananchi wameshiriki kikamilifu katika zoezi la kuchimba msingi wa majengo hayo, wakionesha ari ya kushirikiana na serikali katika kuharakisha utekelezaji wa mradi huo muhimu kwa maendeleo ya elimu katika kata hiyo huku wakieleza kuwa awali walifikiria kuchangishana kuanza ujenzi hivyo fedha hiyo imewapunguzia gharama.

Nao baadhi ya wanafunzi wamesema madarasa hayo itakuwa ni utatuzi wa wanafunzi wengi kulundikana madarasani.