Pambazuko FM Radio

Lishe mbinu mojawapo kukuza ufaulu Lumemo

6 February 2026, 8:02 pm

Picha ya Wanafunzi katika shule ya Msingi Kigamboni(Picha na Katalina Liombechi)

Suala la lishe tumekubalina kwenye vikao na mikutano hivyo tunaendelea kukumbushana na kuhimizana”

Na Katalina Liombechi

Viongozi na Wananchi kata ya Lumemo katika Halmashauri ya Mji wa Ifakara wameendelea kuhamasishana kuchangia lishe mashuleni ili kuwasaidia watoto kujifunza bila vikwazo.

Hayo yamesemwa na Diwani wa Kata hiyo, Mheshimiwa Frank Moses Ngao, wakati akizungumza na Pambazuko FM ofisini kwake.

Mheshimiwa Ngao amesema suala la lishe limekubalika kwa pamoja kati ya uongozi wa kata na wazazi kupitia vikao na mikutano mbalimbali, huku akisisitiza kuwa juhudi za kuhimiza ushiriki wa wazazi zinaendelea.

Picha ya Mh.Frank Ngao Diwani kata ya Lumemo(Picha na Katalina Liombechi)
Sauti ya Diwani Frank Ngao

Kwa upande wake, Mwalimu Mkuu Msaidizi wa Shule ya Msingi Kigamboni, Michael Mkemwa, amesema licha ya baadhi ya wazazi kujitokeza vizuri kuchangia lishe, bado wapo wachache wenye mwitikio mdogo hali inayowasababishia baadhi ya wanafunzi kushindwa kujifunza kwa umakini, kusinzia darasani na wakati mwingine kukumbwa na utoro.

Picha ya Michael Mkemwa Mwalimu Mkuu Msaidizi shule ya Msingi Kigamboni(Picha na Katalina Liombechi)
Sauti ya Mwalimu Mkuu Msaidizi shule ya Msingi Kigamboni

Naye mmoja wa wazazi katika Kata ya Lumemo ametoa wito kwa wazazi wenzake kuona umuhimu wa kuchangia lishe, akisisitiza kuwa ni jukumu lao la msingi kwa ustawi wa watoto wao.

Sauti ya Mzazi Kata ya Lumemo

Wakati huo huo, baadhi ya wanafunzi wa Shule za Msingi Kigamboni na Lumemo wamesema hawajisikii vizuri kuona wenzao wakikosa chakula wanapokuwa shuleni, wakieleza kuwa hali hiyo huathiri ujifunzaji wao.

Picha ya Mwanafunzi Shule ya msingi Kigamboni(Picha na Katalina Liombechi)
Sauti za Wanafunzi Shule za msingi Kigamboni na Lumemo