Pambazuko FM Radio
Pambazuko FM Radio
25 October 2025, 10:01 am

TANAPA yafunga Tembo kifaa maalum (collar) kudhibiti uharibifu wa mazao unaofanywa na wanyama pori katika vijiji vinavyozunguka Hifadhi ya Nyerere, wilayani Kilombero.
Na; Isidory Mtunda
Mamlaka ya Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA) imefanikiwa kumfunga Tembo mmoja kifaa kinachojulikana kama kisukuma mawimbi (collar) katika Hifadhi ya Taifa ya Nyerere, kijiji cha Katurukila, kata ya Mkula, wilaya ya Kilombero, mkoani Morogoro. Hatua hiyo inalenga kudhibiti Tembo wanaoingia mashambani na kuharibu mazao ya wananchi.

Afisa Mhifadhi Daraja II na Msimamizi wa Kanda ya Msolwa, George Baraka, amesema lengo ni kuyafikia makundi matatu ya Tembo ambao wameonekana kuwa hatarishi katika maeneo yanayozunguka hifadhi hiyo, ambapo mara kwa mara wamekuwa wakiharibu mazao na kusababisha hofu kwa wananchi.

Kwa upande wao, mwenyekiti wa kijiji cha Katurukila, Athuman Kayoga, na mtendaji wa kijiji, Bright Mwinyi, wamesema uwepo wa tembo hao umekuwa kikwazo kwa shughuli za kila siku za wananchi.
Ambapo wameeleza kuwa wanyama hao huingia kijijini hata saa 12 asubuhi, jambo linalowazuia wakulima kwenda mashambani na watoto kuhudhuria masomo shuleni.
Maeneo mengi yanayozunguka hifadhi za taifa nchini Tanzania hukumbwa na changamoto ya wanyama pori kuvamia makazi na mashamba ya wananchi. TANAPA imeanza kutumia teknolojia ya “GPS collaring” kufuatilia mienendo ya wanyama hatarishi kwa lengo la kupunguza migogoro kati ya binadamu na wanyama pori, hasa katika maeneo yanayozungwa na hifadhi.