Pambazuko FM Radio
Pambazuko FM Radio
23 September 2025, 6:33 pm

Wakulima Ifakara wamefundishwa umuhimu wa kupima udongo na kutumia mbolea kulingana na mahitaji halisi ya udongo.
Na; Isidory Mtunda
Wakulima katika halmashauri ya mji wa Ifakara, wilaya ya Kilombero, wamepatiwa mafunzo juu ya kanuni bora za kilimo, hususan umuhimu wa kupima afya ya udongo kabla ya kupanda mazao.
Emanueli Kadilo, Afisa Kilimo wa Halmashauri ya mji wa Ifakara, amesema kuwa kupitia upimaji wa afya ya udongo, wakulima wataweza kutambua mahitaji halisi ya mashamba yao, jambo litakalosaidia kupunguza gharama za uzalishaji na kuhakikisha matumizi sahihi ya virutubisho.

Akiongeza juu ya mada hiyo, Edwin Shio, Afisa Kilimo kutoka Farm Africa kupitia mradi wa Farm to Market Alliance, amesema wakulima wamefundishwa pia kuhusu namna ya kuongeza rutuba kwenye udongo, matumizi sahihi ya viuatilifu, pamoja na kuachana na mazoea yasiyo na tija kwenye kilimo.

Kwa upande wao, wakulima Merina Luyanji na Jafreda Kashabano wamesema mafunzo hayo yamewasaidia kuelewa kuwa upimaji wa udongo ni hatua muhimu kabla ya kutumia mbolea, badala ya kutumia kiholela kama ilivyokuwa awali.
Naye Asumtha Lipindu, mtaalamu wa afya ya udongo kutoka kampuni ya Bizy Tech, amesisitiza kuwa uzalishaji wa tija unategemea mbegu bora, virutubisho sahihi na ushauri kutoka kwa maafisa kilimo waliobobea, akiwashauri wakulima kushirikiana na wataalamu katika kila hatua.

Akifunga mafunzo hayo, Thomas Mbega, Mratibu wa mradi wa Farm to Market Alliance, amesema changamoto kubwa wanayoikuta ni wakulima kuomba mbegu wakiwa wamechelewa, hali inayowafanya kukosa msaada kwani taasisi kama TARI huwa tayari zimekamilisha ugavi wa mbegu hizo.
Sauti ya bwana Thomas Mbega