Pambazuko FM Radio

SIDO yatunuku vyeti wajasiriamali 250

18 September 2025, 11:05 pm

Mariam Mmbaga mmoja wa washiriki wakipokea cheti – Picha na; Jackline Jerome

SIDO yamaliza mafunzo ya siku 3 kwa wajasiriamali 250 Kilombero na kutunuku vyeti; DC atoa agizo la kufunguliwa kwa ofisi ya SIDO wilayani humo kusogeza huduma karibu na wananchi.

Na; Isidory Mtunda

Washiriki 250 wa semina ya wajasiriamali, wawekezaji na wenye viwanda katika Wilaya ya Kilombero wamehitimu mafunzo ya siku tatu na kutunukiwa vyeti vya ushiriki kutoka Shirika la Kuhudumia Viwanda Vidogo (SIDO).

Akifunga mafunzo hayo, Mkuu wa Wilaya ya Kilombero, Wakili Dunstan Kyobya, amelielekeza shirika hilo kufungua ofisi katika wilaya hiyo ili kusogeza huduma kwa wananchi wa Kilombero, Malinyi na Ulanga, na kuwapunguzia adha ya kusafiri hadi makao makuu ya SIDO mjini Morogoro.

Mkuu wa wilaya ya Kilombero – wakili Dunstan Kyobya (mwenye microphone) – Picha na; Jackline Jerome
sauti ya mkuu wa wilaya – Dunstan Kyobya

Meneja wa SIDO Mkoa wa Morogoro, Bi. Joan Nangawe, amepongeza agizo hilo akisema litasaidia kuongeza ufanisi wa utoaji huduma kwa wajasiriamali, kwani kwa sasa wamekuwa wakihudumiwa kwa uchache kutokana na ukosefu wa ofisi ya kudumu katika eneo hilo.

Meneja wa SIDO – Morogoro – Joane Nangawe ( mwenye microphone) – Picha na; Jackline Jerome
sauti ya Joan Nangawe – meneja wa SIDO Morogoro

Kwa upande wake, Afisa Maendeleo wa Halmashauri ya Mji wa Ifakara, Bi. Mercy Gibson Minja, amesema tayari wameanza utekelezaji wa agizo la Mkuu wa Wilaya kuhusu kugawa vitambulisho 250 kwa wajasiriamali waliohitimu, ambapo ndani ya mwezi mmoja na nusu kila mmoja anatarajiwa kuwa amepokea kitambulisho chake.

Mercy Minja – afisa maendeleo Ifakara mji – Picha na: Jackline Jerome
Sauti ya afisa maendeleo – Mercy Minja

Akizungumza kwa niaba ya washiriki, Mariamu Mmbaga amesema elimu waliyoipata imewasaidia kujua umuhimu wa kurasimisha biashara na kuacha kufanya shughuli kienyeji. Pia amepongeza ushauri walioupata kutoka Shirika la Viwango Tanzania (TBS) kuhusu uhitaji wa nembo za ubora kwenye bidhaa zao.

Marimu Mmbaga mmoja wa washiriki – Picha na: Jackline Jerome
Sauti ya Mariamu Mmbaga