Pambazuko FM Radio

Mkopo wa WBN kuwainua wajasiriamali wadogo

8 July 2025, 7:05 pm

Picha ya Esther Mtweve (kulia)Afisa maendeleo ya Jamii akimsajili Mjasiriamali kwenye mfumo(Picha na Katalina Liombechi)

Athari za mikopo isiyo rafiki hasa kwa wajasiriamali wadogo wengi hujikuta wakishindwa kulipa mikopo hiyo kwa wakati kutokana na viwango vya riba visivyodhibitika na hatimaye kudumaa zaidi kiuchumi

Na Katalina Liombechi

Imeelezwa kuwa Mikopo yenye riba kubwa maarufu kama chap chap imekuwa ikiwatesa wajasiriamali wadogo hali inayopelekea kuadhirika na wengine kukimbia na kutelekeza familia.

Baadhi ya wajasiliamali wadogo wananchi wa kitongoji cha uwanja wa ndege kata ya Kibaoni Tunu Kipendawazungu na Issa Siraji wameyasema hayo wakati wakizungumza na Pambazuko FM katika zoezi la kuwaandikisha wajasiliamali kwenye mfumo ili waweze kunufaika na mikopo kwa Wajasiliamali isiyo na riba ambayo inayotolewa na Serikali kupitia benki ya NMB.

Wananchi hao wamesema changamoto ya mikopo hiyo imekuwa ikifilisi watu na wakisalia kwenye hali duni hivyo ujio wa fursa ya mikopo hiyo itawakwamua zaidi kiuchumi.

Picha ya Tunu Kipendawazungu Mjasiriamali(Picha na Katalina Liombechi)
Sauti ya wajasiliamali Uwanja wa Ndege

Akizungumzia zoezi hilo na sifa za kunufaika na mikopo hiyo Afisa maendeleo ya jamii kata ya Kibaoni bi. Esther Mtweve amesema mikopo hiyo inayojulikana kama WBN  imekuja wakati mwafaka na Serikali ya Dkt Samia imekusudia vyema kuwaondoa wananchi katika changamoto ya mikopo umiza.

Picha ya bi Esther Mtweve Afisa maendeleo ya jamii Kibaoni(Picha na Katalina Liombechi)
Sauti ya bi Esther Mtweve Afisa maendeleo ya jamii Kibaoni

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Kitongoji hicho Bwana Jeremiah Machibya amesema hiyo ni fursa adhimu kwa wananchi wake huku akiwataka kujitokeza kwa wingi kusajiliwa na hatimaye kupata mikopo itakayowasaidia kukuza mitaji yao.

Picha ya Jeremiah Machibya Mwenyekiti kitongoji cha uwanja wa Ndege(Picha na Katalina Liombechi)
Sauti ya Jeremiah Machibya Mwenyekiti

Zoezi la kuwasajili wajasiliamali wadogo kwenye mfumo linafanyika katika Wilaya nzima ya Kilombero na katika kitongoji cha Uwanja wa Ndege linafanyika katika shule ya Msingi Uwanja wa Ndege.