Pambazuko FM Radio

Zaidi ya asilimia 90 Ifakara wamelipa kodi

26 June 2025, 10:44 pm

Picha ya Maafisa wa TRA wakiwa katika ofisi ya DC Kilombero(Picha kwa hisani ya Nuruh Kilawe)

Kwa eneo hili Ifakara wengi wamekwishalipa kodi tunaendelea kuwahimiza

Na Katalina Liombechi

Timu ya Maafisa wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) kupitia Makao Makuu kwa kushirikiana na ofisi ya TRA mkoa wa Morogoro, imeendelea na  ziara yake maalum katika mji wa Ifakara wilayani Kilombero, kwa lengo la kuwatembelea walipakodi, kusikiliza changamoto zao na kuwakumbusha umuhimu wa kulipa kodi kwa maendeleo ya Taifa.

Wakiwa Katika ziara hiyo leo, timu hiyo imebaini changamoto kadhaa zinazowakabili wafanyabiashara, kubwa ikiwa ni malalamiko kuhusu uelewa wa matumizi na matengenezo mashine za EFD pale zinapoharibika jambo ambalo limekuwa kero kwao kama navyoeleza mmoja wa wafanyabiashara Ifakara.

sauti ya Christopher Mwita Mfanyabiashara

Kufuatia kero hiyo, timu hiyo ya TRA ilifika kwa wakala wa mashine za EFD, Bw. Jeremiah Machibya, kupata ufafanuzi juu ya suala hilo na kwamba Machibya ameeleza kuwa baadhi ya gharama hizo zinatokana na huduma na vipuri vinavyohitajika wakati wa matengenezo, huku akieleza muda mwingine wafanyabiashara wamekuwa wakitengeneza mazingira ya kujitetea.

sauti ya wakala akihojiwa na Afisa wa TRA

Akizungumza katika ziara hiyo, Afisa Mwandamizi Msimamizi wa Kodi kutoka TRA mkoa wa Morogoro, Bi. Immaculate Chaggu, amesema kuwa zaidi ya asilimia 90 ya wafanyabiashara wa Ifakara tayari wamelipa kodi zao, jambo linaloashiria uelewa na ushirikiano mkubwa kutoka kwa walipakodi.

Picha ya Maafisa wa TRA(Picha kwa hisani ya Nuruh Kilawe)
sauti ya Afisa wa TRA Morogoro

Kwa upande wao, baadhi ya walipakodi waliozungumza na redio Pambazuko FM wamesema wamefurahishwa na huduma zinazotolewa na TRA kwa sasa, wakieleza kuwa ni rafiki zaidi ukilinganisha na miaka ya nyuma.

sauti ya walipa kodi Ifakara

Ziara hiyo iliyoanza Juni 23,2025 ambayo ni maelekezo ya Kamishina General wa Mamlaka hiyo ni sehemu ya mkakati wa TRA kuimarisha mahusiano na walipakodi, kutatua changamoto kwa haraka na kuhakikisha kila mfanyabiashara anatimiza wajibu wake wa kulipa kodi kwa hiari.