Pambazuko FM Radio

DC Kyobya akemea vitendo vya ukatili dhidi ya watoto

16 June 2025, 8:24 pm

Picha ya watoto katika maadhimisho siku ya Mtoto wa Afrika Ifakara(Picha na Katalina Liombechi)

Lengo kubwa ni kumlinda mtoto aweze kutimiza ndoto zake,tunataka kila mtoto asome

Na Katalina Liombechi

Wazazi na Jamii Wilayani Kilombero wametakiwa kuzifanyia kazi changamoto zinazowakabili watoto kama vitendo vya ukatili na wazazi kutoa ushirikiano katika malezi na lishe ili waweze kutimiza ndoto zao.

Haya yanakuja baada ya Watoto kuwasilisha changamoto zao kupitia risala yao katika Maadhimisho ya Mtoto wa Afrika ambapo katika Halmashauri ya Mji wa Ifakara Maadhimisho hayo kwa mwaka 2025 yamefanyika katika shule ya Msingi Kiningina, yakihudhuriwa na mamia ya wanafunzi, walimu, wazazi na wadau wa maendeleo ya watoto.

Katika risala hiyo iliyosomwa na wanafunzi Shaban Hassan na Rachel Ngalawa kwa niaba ya watoto wenzao wameeleza changamoto mbalimbali zinazowakumba ikiwa ni pamoja na ukosefu wa baadhi ya huduma muhimu, vitendo vya ukatili majumbani na kwenye jamii ambazo wamesema zinakwamisha maendeleo yao ya elimu.

Picha ya Shaban Hassan na Rachel Ngalawa wakikabidhi risala kwa Mgeni rasmi Mh.Kyobya(Picha na Katalina Liombechi)
Sauti ya Shaban Hassan na Rachel Ngalawa

Mgeni rasmi katika maadhimisho hayo Mkuu wa Wilaya ya Kilombero, Wakili Dunstan Kyobya, ambaye ametoa wito kwa jamii kuhakikisha watoto wanalelewa kwa upendo, ulinzi na kupata huduma zote muhimu, ikiwemo elimu, afya na chakula.

Aidha ameahidi kufuatilia kwa karibu masuala yote yaliyowasilishwa na watoto hao, huku akitoa maelekezo kwa idara zinazohusika kuhakikisha hatua stahiki zinachukuliwa kwa haraka.

Picha ya Mh.Dunstan Kyobya Mkuu wa Wilaya ya Kilombero(Picha na Katalina Liombechi)
Sauti ya Mh.Dunstan Kyobya Mkuu wa Wilaya ya Kilombero

Kwa upande wake, Mkuu wa Idara ya Maendeleo ya Jamii katika Halmashauri ya Mji wa Ifakara, Bi Florence Mwambene, alisema kuwa ofisi yake imepokea kwa uzito mkubwa maagizo yaliyotolewa na Mkuu wa Wilaya, na kueleza kuwa utekelezaji wake unahitaji ushirikiano wa karibu kutoka kwa wadau mbalimbali.

Picha ya Bi.Florence Mwambene Mkuu wa Idara ya Maendeleo ya jamii Ifakara(Picha na Katalina Liombechi)
Sauti ya Bi.Florence Mwambene Mkuu wa Idara ya Maendeleo ya jamii Ifakara

Baadhi ya Wazazi waliohudhuria katika maadhimisho hayo pamoja naye Mwalimu Avit Mosha kutoka Shule ya sekondari Kilombero wamekiri kuwepo kwa changamoto zinazokwamisha maendeleo yao na kwamba wako tayari kuzifanyia kazi.

Picha ya baadhi ya wazazi waliohdhuria maadhimisho ya siku ya Mtoto wa Afrika(Picha na Katalina Liombechi)
Sauti ya baadhi ya wazazi na Mwalimu

Siku ya Mtoto wa Afrika huadhimishwa kila mwaka tarehe 16 Juni kwa lengo la kukumbuka mauaji ya kikatili ya watoto waliokuwa wakidai haki yao ya elimu nchini Afrika Kusini mwaka 1976, na kuchochea juhudi za kutetea na kulinda haki za watoto kote barani Afrika ambapo mwaka huu 2025 kauli mbiu inasema “Haki ya Mtoto:tulipotoka,tulipo na tuendako”