Pambazuko FM Radio
Pambazuko FM Radio
31 January 2025, 6:49 pm
Na Katalina Liombechi

Serikali yetu imeweka mifumo rahisi ya ulipaji kodi nasi tumekuwa tukisikiliza changamoto za wafanyabiashara na kuzitatua kwa wakati.
Mamlaka ya Mapato Tanzania TRA Wilaya ya Kilombero Imesema itaendelea kutatua changamoto za wafanyabishara na kuweka Mazingira rafiki ya Ulipaji wa Kodi ili Kufikia malengo ya Serikali katika Ukusanyaji wa Mapato.
Meneja wa Mamlaka hiyo wilaya ya Kilombero Wilfred Makamba amesema hayo hii leo January 31,2025 katika kikao cha kuwapongeza wafanyabiashara mfano kwa kulipa kodi kama Serikali inavyoelekeza kikao ambacho kimefanyika katika Ukumbi wa Ofisi ya Bonde la Rufiji Kilombero kikiongozwa na Mkuu wa Wilaya ya Kilombero wakili Dunstan Kyobya ambaye ndiye Mwenyekiti wa Kodi katika Wilaya hiyo.
Amesema wamekuwa wakifikia malengo ya ukusanyaji wa Mapato kutokana na utaratibu mzuri wa kutoa elimu ya Mara kwa mara,kuwafikia Wafanyabiashara mmoja mmoja,kujadiliana juu ya Changamoto zao na kuzitatua kwa wakati pia TRA Wametoa tuzo kwa wafanyabiashara Kessy hard ware na Missionaries of Compassion huku akiomba Ushirikiano zaidi.

Mh.Kyobya amesema Mafanikio ya kibiashara na Ulipaji kodi kwa wakati unachagizwa na Miundombinu rafiki ya Uwekezaji,kuondolewa vikwazo kwa Wafanyabiashara ambapo pamoja na mambo mengine ametumia kikao hicho kuwaalika Wafanyabiashara wengine kutoka ndani na nje ya Kilombero kuja Kuwekeza.

Mfanyabiashara Didas Kessy (Kessy Hard ware amesema wanajivunia ushirikiano wanaoupata kutoka kwa mamlaka hiyo na serikali huku akiwaomba Wafanyabiashara wenzake kuwa na kawaida ya kuzungumza na TRA wanapokutana na changamoto badala ya kutengeneza Mazingira ya kukwepa kodi.

Kumbuka TRA ina majukumu ya kukusanya Kodi,kusimamia Sheria za kodi,kupambana na uvunjaji wa Sheria za kodi,kutoa huduma kwa walipa kodi,kutafiti na kufanya uchambuzi wa kiuchumi,kusimamia mfumo wa Forodha pamoja na kutoa leseni na vibali.