Boma Hai FM

Waalimu Masama Magharibi wapongezwa, Dc Bomboko ataka mapinduzi ya elimu

5 March 2026, 9:10 am

Pichani ni mkuu wa wilaya ya Hai Hassan Bomboko akimkabidhi cheti cha pongezi mwalimu Agrey Mrema(picha na Elizabeth Mafie)

Katika hafla ya kuwapongeza walimu wa kata ya Masama Magharibi iliyofanyika Machi 3, 2026 mkuu wa wilaya ya Hai Hassan Omar Bomboko, amesisitiza umuhimu kuandaliwa kwa mpango kazi madhubuti wa kitaaluma ili kuongeza ufaulu wa wanafunzi wa shule za msingi na sekondari, akitaja nidhamu, ubunifu na matumizi ya TEHAMA kuwa nguzo muhimu za elimu .

Na Elizabeth Mafie & Stanley Christian.

Hai-Kilimanjaro

Mkuu wa wilaya  ya Hai  Hassan Omar Bomboko amewataka wataalamu wa elimu wilaya ya Hai mkoani Kilimanjaro  kuandaa mpango kazi madhubuti wa kitaaluma utakaosaidia kuimarisha ubora wa ufundishaji  Ili kuendelea kuongeza ufaulu wa wanafunzi katika shule za msingi na sekondari za wilaya ya Hai.

Pichani ni afisa elimu kata ya Masama Magharibi Mwalimu Raymond Mchome akisoma risala wakati wa hafla ya kuwapongeza waalimu wa kata hiyo.(picha na Elizabeth Mafie)

Bomboko ametoa wito huo  Machi 3, 2026 akiwa mgeni rasmi katika hafla ya kuwapongeza walimu wa Kata ya Masama Magharibi kwa matokeo mazuri ya kitaaluma, akisisitiza umuhimu wa nidhamu, ubunifu pamoja na matumizi sahihi ya TEHAMA ili kuendana na mabadiliko ya elimu ya kisasa.

Sauti ya mkuu wa wilaya ya Hai Hassan Omar Bomboko

Kwa upande wake afisa elimu wa Kata ya Masama Magharibi Raymond Mchome, amesema mafanikio yaliyopatikana ni matokeo ya ushirikiano mzuri kati ya walimu, wazazi na uongozi wa kata na kwamba  juhudi zinaendelea kuboresha miundombinu ya shule na kuongeza upatikanaji wa vifaa vya kufundishia pamoja na TEHAMA ili kuinua zaidi kiwango cha elimu na kamba mshikamano wa wadau wa elimu utaendelea kuwa chachu ya maendeleo ya taaluma katika kata hiyo.

Baadhi ya waalimu wa kata ya Masama Magharibi wakiwa katika hafla ya kupongezwa kutokana na na shule wanazofundisha kufanya vizuri katika mitihani mbalimbali.(picha na Elizabeth Mafie)

Nae diwani wa kata hiyo Eliufoo Happy Christopher, amesema uongozi wa kata unaendelea kuweka mikakati ya kutambua mahitaji ya shule na kuyafanyia kazi kwa hatua za muda mfupi na muda mrefu, kwa lengo la kudumisha na kuongeza mafanikio yaliyopo.

Sauti ya diwani wa kata ya Masama Magharibi Eliufoo Happy Christopher,

 Hata hivyo waalimu waliopongezwa wameahidi kuendelea kufanya kazi kwa bidii, kuzingatia maadili ya taaluma na kutumia mbinu bunifu za ufundishaji ili kuimarisha zaidi matokeo ya wanafunzi na kudumisha heshima ya elimu katika Wilaya ya Hai.

Pichani ni mkuu wa wilaya ya Hai Hassan Omar Bomboko (aliyesimama)akizungumza katika hafla ya kuwapongeza waalimu wa kata ya Masama Magharibi(picha na Elizabeth Mafie)

Hafla hiyo imeandaliwa na Ofisi ya Diwani wa Kata ya Masama Magharibi kwa kushirikiana na Ofisi ya Afisa Elimu Kata, ikiwa ni sehemu ya kutambua na kuthamini mchango wa walimu katika maendeleo ya elimu.

Pichani ni mkuu wa wilaya ya Hai Hassan Omar Bomboko akimkabidhi kombe la ushindi mwalimu mkuu wa shule ya sekondari Kyuu Lightness Mlula(picha na Elizabeth Mafie)