Boma Hai FM
Boma Hai FM
26 February 2026, 1:20 pm

Baraza la madiwani halmashauri ya wilaya ya Hai mkoani Kilimanjaro limepitisha bajeti ya zaidi ya shilingi bilioni hamsini na mbili kwa mwaka wa fedha 2026/2027.
Na Elizabeth Mafie
Hai – Kilimanjaro
Mwenyekiti wa Halmashauri ya wilaya ya Hai mkoa wa Kilimanjaro Edmund Rutaraka, amesema baraza la madiwani limepitisha bajeti ya zaidi ya shilingi bilioni 52 kwa mwaka wa fedha 2026/2027, itakayolenga kuimarisha huduma za elimu, afya pamoja na miundombinu ya barabara katika wilaya ya Hai.
Bajeti hiyo imeidhinishwa februari 25, 2026 katika kikao maalumu cha baraza la madiwani kilichofanyika katika ukumbi wa Halmashauri ya wilaya ya Hai, ambapo msisitizo umewekwa katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo itakayochochea ukuaji wa uchumi na kuboresha maisha ya wananchi.

Akiwasilisha mapendekezo ya mpango na bajeti kwa niaba ya Mkurugenzi Mtendaji, Afisa Mipango na uratibu wa halmashauri, Saidi Abdalah amesema fedha hizo zitaelekezwa katika ujenzi na ukarabati wa shule, vituo vya afya pamoja na barabara za ndani ili kurahisisha upatikanaji wa huduma muhimu kwa wananchi.
Baadhi ya madiwani walichangia hoja mbalimbali wakisisitiza usimamizi makini wa miradi na matumizi sahihi ya fedha za umma ili kuhakikisha malengo yaliyopangwa yanafikiwa kwa ufanisi.
Akizungumza kwa niaba ya Katibu Tawala wa Mkoa wa Kilimanjaro, Gasper Ijiko amehimiza uwajibikaji na ushirikiano katika utekelezaji wa miradi hiyo, huku wananchi wakihimizwa kushiriki kikamilifu katika kulinda na kutunza miundombinu inayojengwa.

Akifunga kikao hicho, Mwenyekiti wa halmashauri ya wilaya ya Hai, Edmund Rutaraka amewataka madiwani na wataalamu kuongeza juhudi katika kusimamia miradi ya maendeleo ili bajeti iliyopitishwa iweze kuleta matokeo chanya kwa wananchi.