Boma Hai FM

Bodi ya Maji Uroki Bomang’ombe yahitimisha ukaguzi na tathmini ya miundombinu

29 November 2025, 10:01 am

Pichani ni Mhandisi Rogers Marandu(kushoto)pamoja na mwenyekiti wa Bodi ya Uroki Bomang’ombe Batista Mngullu wakiwa katika kikao cha tathmini ya ukaguzi wa miundombinu ya bodi hiyo.(picha na Elizabeth Mafie)

Bodi ya Maji Uroki Bomang’ombe imehitimisha ukaguzi wa kila mwaka wa vyanzo na miundombinu ya maji katika Wilaya ya Hai, lengo ikiwa ni kuhakikisha miradi ya maji inakuwa endelevu na maji yanayotolewa kwa wananchi ni salama, na huduma ya maji inaendelea kuboreshwa.

Na Elizabeth Mafie Hai -Kilimanjaro

Kufanya ukaguzi wa mara kwa mara kwenye vyanzo vya maji  pamoja na miundombinu husaidia kubaini maeneo yenye changamoto na kuweka mikakati ya kuboresha huduma kwa wananchi.

Pichani ni baadhi ya watumishi wa Bodi ya Maji Uroki Bomang’ombe pamoja na wageni waalikwa wakiwa katika kikao cha tathmini ya ukaguzi wa miundombinu ya bodi hiyo(picha na Elizabeth Mafie)

Akizungumza Novemba 28 ,2025 katika kikao cha tathmini ya ukaguzi wa miundombinu kilichofanyika katika Ofisi za Bodi ya Maji Uroki Bomang’ombe kata ya Romu wilayani Hai mkoani Kilimanjaro, Mhandisi Rogers Marandu amesema tathmini hiyo inalenga kuhakikisha miradi ya maji inabaki kuwa endelevu huku akisisitiza  kuwa ukaguzi wa mara kwa mara unasaidia kubaini maeneo yenye changamoto na kuweka mikakati ya kuboresha huduma kwa wananchi.

Pichani ni wageni waalikwa wakiwa katika kikao cha tathmini ya ukaguzi wa miundombinu ya Bodi ya maji Uroki Bomang’ombe(picha na Elizabeth Mafie)

Ameeleza kuwa katika tathmini hiyo wamekuwa wakichunguza kwa kina ubora wa maji kwa kuhakikisha yanayotoka kwenye vyanzo na mitandao ya usambazaji ni safi na salama kwa matumizi ya binadamu. Aidha, ukaguzi huo unahusisha kufuatilia matumizi ya dawa zinazotumika kutibu maji ili kubaini iwapo zinatumika kwa usahihi na kwa kiwango kinachotakiwa.

Pichani ni Mhandisi Anord Mbaruku ambae ndie meneja wa Bodi ya maji Uroki Bomang’ombe akiwa katika kikao cha tathmini ya ukaguzi wa miundombinu ya bodi hiyo(picha na Elizabeth Mafie)

Amesema hatua hizi  ni muhimu katika kulinda afya za wananchi na kuhakikisha huduma inayotolewa inakidhi viwango vinavyotakiwa.

Pichani ni Dkt Aloyce Leole ambae anapata huduma ya maji kutoka bodi ya maji Uroki Bomang’ombe(picha na Elizabeth Mafie)

Mhandisi Marandu ameongeza kuwa timu hiyo imekuwa ikitembelea miundombinu ya maji ili kujiridhisha kama ipo salama na kufanya kazi ipasavyo, sambamba na kuainisha makosa na dosari zilizojitokeza katika mwaka husika  na kwamba taarifa hizo hutumika kupanga marekebisho na maboresho kwa msimu ujao ili kuhakikisha mfumo wa usambazaji maji unaendelea kuwa imara, thabiti na wenye manufaa kwa jamii ya Wilaya ya Hai.

Sauti ya Mhandisi Rogers Marandu

Kwa upande wake mwenyekiti wa Bodi ya Maji Uroki Bomang’ombe, Batista  Mngullu  amesema kupitia tathmini hiyo wamejifunza kusema ukweli, kutambua makosa na kuyafanyia maboresho huku akitoa rai kwa watumishi wote wa Bodi ya Maji Uroki kuwa na ari ya utendaji ili kuendelea kuwa bodi bora na ya mfano katika utoaji wa huduma kwa jamii.

Sauti ya mwenyekiti wa Bodi ya maji Uroki Bomang’ombe Batista Mngullu

Wakizungumza katika kikao hicho  baadhi ya watumia maji wa bodi hiyo wamesema ushirikishwaji wa jamii husaidia bodi kupata taarifa mapema iwapo kuna chanzo kimepata hitilafu huku wakiipongeza Bodi ya Maji Uroki Bomang’ombe kwa juhudi za kudhibiti magonjwa hatari yanayosababishwa na maji yasiyo salama kama typhoid, kipindupindu, polio na amoeba.

Sauti ya Dr Aloyce Leole na Rogath Mushi ambae ni mjumbe wa kamati ya maji kijiji cha Shari.