Boma Hai FM

HRT SACCOS yazidi kung’ara, yarudisha kwa jamii

22 July 2025, 8:40 pm

Pichani ni madawati arobaini yaliyokabidhiwa katika shule ya msingi Ngare Mji na HRT SACCOS (picha na Elizabeth Noel)

 “Mhe mkuu wa wilaya kila mwaka chama kinatekeleza msingi wa saba wa ushirika kwa kuendelea kuijali jamii,na mwaka huu Mh mkuu wa wilaya tumetembelea shule hii ya  msingi Ngare Mji na tunatoa madawati ambayo thamani yake ni shilingi milioni 4 ,mwaka huu chama kinaadhimisha miaka 25 tangu kuanzishwa”

Na Elizabeth Noel Siha –Kilimanjaro

Chama cha Akiba na Mikopo Hai Rural Teachers Saccos (HRT)kimekabidhi madawati 40 yenye thamani ya kiasi cha shilingi milioni nne katika shule ya Ngare Mji iliyopo wilayani Siha Mkoani Kilimanjaro.

HRT Saccos imekabidhi madawati hayo Julai 22,2025 ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa  msingi wa saba wa vyama vya ushirika unaohimiza   kurudisha kwa jamii faida inayopatikana ndani ya chama.

Pichani ni mwakilishi wa mkuu wa wilaya ya Siha Shedrack Moshi(katikati) na mwenyekiti wa HRT SACCOS Mwalimu Alex Warioba (aliyevaa miwani) pamoja na kaimu mkurugenzi mtendaji halmashauri ya wilaya ya Siha Dr Paschal Mbota(picha na Elizabeth Noel)

Akizungumza wakati wa kupokea madawati hayo mwakilishi wa mkuu wa wilaya ya Siha Shedrack Moshi ameishukuru HRT SACCOS kwa jitihada walizofanya na kuona umuhimu wa kurudisha kwa jamii na kwamba madawati hayo yanakwenda kuondoa msongamano wa wanafunzi darasani na kufanya ufaulu kuongezeka

Pichani ni Uongozi wa HRT SACCOS na mrajisi msaidizi wa vyama vya ushirika mkoa wa Kilimanjaro Jacklin Senzighe (kulia) wakikabidhi madawati kwa mwakilishi wa mkuu wa wilaya Siha pamoja na kaimu mkurugenzi wa wilaya hiyo.(picha na Elizabeth Noel)

“Ndugu zangu nipende kusema kwa niaba ya serikali kwamba tumefarijika sana na jitihada hizi ambazo zimefanywa na chama hiki ambacho kimeona umuhimu wa kurudisha kwa jamii,na leo hii wamekabidhi madawati 40 kwa ajili ya watoto wetu katika shule hii,badala ya watoto kukaa kwa kusongamana sasa hivi wataweza kukaa vizuri na hivyo ule usikivu na kama alivyohaidi mwalimu mkuu ufaulu unaenda kuongezeka”Amesema Moshi

Sauti ya mwakilishi wa mkuu wa wilaya ya Siha Shedrack Moshi.

Awali akisoma taarifa ya HRT SACCOS  Mwalimu Alex Warioba ambae ni mwenyekiti wa chama hicho amesema kila mwaka chama kinatekeleza msingi wa saba wa vyama vya ushirika kwa kuendelea kuijali jamii na kwa mwaka 2025 wameona ni vyema kutoa madawati hayo ili  kupunguza upungufu wa madawati uliopo katika shule hiyo.

 “Mh mkuu wa wilaya kila mwaka chama kinatekeleza msingi wa saba wa ushirika kwa kuendelea kuijali jamii,na mwaka huu Mh mkuu wa wilaya tumetembelea shule hii ya  msingi Ngare Mji na tunatoa ambayo thamani yake ni shilingi milioni 4 ,mwaka huu chama kinaadhimisha miaka 25 tangu kuanzishwa”Amesema Mwalimu Warioba.

Sauti ya mwenyekiti wa HRT SACCOS mwalimu Alex Warioba.

Nae afisa elimu msingi wilaya ya Siha Fatu Msangi amesema kupitia msaada huo wa madawati yaliyotolewa na HRT SACCOS yatafanya utekeleza wa mtaala kufanyika kwa ufanisi zaidi.

Pichani ni meneja wa HRT SACCOS Upendo Lyatuu (katikati) na Mrajisi msaidizi wa vyama vya ushirika Mkoa wa Kilimanjaro Jacklin Senzighe (kushoto) pamoja na mwanachama wa HRT SACCOS Happyness Kaaya wakiwa katika nyuso za furaha mara baada ya kukabidhi madawati. (picha na Elizabeth Noel)

“Thamani hizi mlizotupatia zitatufanya utekelezaji wa mtaala kufanyika kwa ufanisi zaidi kuliko ambavyo watoto wangekuwa wamesongamana hivyo tunawashukuru sana HRT SACCOS”Amesema Msangi

Sauti ya afisa elimu msingi wilaya ya Siha Fatu Msangi.

Kwa upande wao wanafunzi wa shule ya msingi Ngare Mji Sofia Yusuph na Asia Hussen wameishukuru HRT SACCOS na kuhaidi kutunza madawati hayo pamoja na kusoma kwa bidii.

Sauti za wanafunzi wa shule ya msingi Ngare Mji Sofia Yusuph na Asia Hussen

Katika wiki ya maadhimisho ya miaka 25 ya  HRT SACCOS imeendesha shughuli mbalimbali za kijamii ikiwemo michezo ya bonanza, kutoa elimu kwa jamii kupitia vyombo vya habari, na sasa kukabidhi madawati hayo kama sehemu ya mchango wake kwa maendeleo ya elimu nchini.