Boma Hai FM
Boma Hai FM
18 July 2025, 8:10 am

Lengo letu ni kuhakikisha wafugaji wanapata elimu sahihi na vifaa muhimu kama chanjo ili waweze kufuga kwa tija hii itasaidia kuongeza pato la taifa na la mtu mmoja mmoja”amesema Lekei.
Na Oliva Joel Hai-Kilimanjaro
Zaidi ya kuku 300 wamechanjwa katika uzinduzi rasmi wa kampeni ya chanjo ya mifugo uliofanyika katika kata ya Bondeni wilayani Hai mkoani Kilimanjaro ikiwa ni sehemu ya juhudi za serikali kuwasaidia wafugaji kukabiliana na changamoto za magonjwa ya mifugo ikiwemo kideri na ndui.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Kaimu Mkurugenzi wa Wilaya ya Hai, Bw. David Lekei, amesema kuwa utoaji wa chanjo hizo za ruzuku ni moja ya mikakati ya serikali ya kuinua sekta ya mifugo nchini.
“Lengo letu ni kuhakikisha wafugaji wanapata elimu sahihi na vifaa muhimu kama chanjo ili waweze kufuga kwa tija hii itasaidia kuongeza pato la taifa na la mtu mmoja mmoja”amesema Lekei.
Kwa upande wake mwenyekiti wa serikali ya mtaa wa Kingereka, Dastarn Kimaro, amesema kuwa zoezi hilo limekuja kwa wakati muafaka na kwamba wafugaji wengi wamekuwa wakipata hasara kubwa kutokana na vifo vya mifugo vinavyosababishwa na magonjwa.
“Chanjo hizi zitasaidia kupunguza matatizo ya kiafya kwa mifugo kama kuku na ng’ombe, hivyo kupunguza gharama kwa wafugaji na kuongeza uzalishaji” amesema Kimaro.
Mmoja wa wananchi walionufaika na chanjo hiyo amepongeza serikali kwa kuwafikia wafugaji moja kwa moja na kutoa huduma hiyo bure.
“Hii chanjo imetusaidia sana, gharama zimepungua na sasa tunafuga kwa kujiamini zaidi” amesema mfugaji huyo.
Uzinduzi huu ni sehemu ya kampeni ya kitaifa ya kuboresha sekta ya mifugo kwa kuwajengea uwezo wafugaji kupitia huduma bora za afya ya mifugo na elimu endelevu.