Boma Hai FM

Mbunge Hai aomba matengenezo barabara ya Rundugai-Simanjiro

10 June 2025, 9:48 pm

Mbunge wa Jimbo la Hai Saashisha E. Mafuwe akiuliza swali bungeni kuhusu uharibifu wa Barabara ya Rundugai-Simanjiro (Picha na Bunge)

Mbunge wa Jimbo la Hai Saashisha Mafuwe ameuliza swali bungeni kuhusu lini serikali itachukua hatua ya ukarabati wa barabara ya Rundugai-Simanjiro inayounganisha wilaya ya Hai na Simanjiro

Na Henry Keto.Hai-Kilimanjaro

Mbunge wa Jimbo la Hai, Mheshimiwa Saashisha Mafue, ameonyesha wasiwasi mkubwa kuhusu hali mbaya ya barabara inayounganisha maeneo ya Rundugai, Kambi ya Chokaa mpaka Simanjiro, ambayo kwa sasa haipitiki kutokana na uharibifu mkubwa unaosababishwa na mvua na sababu nyingine.

Mbunge Mafue amesisitiza kuwa hali hii imevuruga mawasiliano kati ya Wilaya za Hai na Simanjiro na kusababisha usumbufu mkubwa kwa wananchi pamoja na shughuli za kiuchumi katika maeneo haya muhimu.

Sauti ya Mbunge wa Jimbo la Hai akiuliza swali kuhusu ukarabati wa barabara ya Rundugai-Simanjaro

Pichani ni Naibu Waziri wa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Mheshimiwa Zainab Katimba (Picha na Bunge)

Akijibu kuhusu changamoto hii, Naibu Waziri wa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Mheshimiwa Zainab Katimba, amesema Serikali inatambua mazingira hayo na inajitahidi kushughulikia matatizo yanayojitokeza kutokana na mvua na uharibifu wa barabara.

Aidha, Naibu Waziri Katimba ameitaka TARURA mkoa wa Kilimanjaro kwa ushirikiano na mameneja wa Manyara na wilaya husika kuhakikisha tathmini ya kina ya uharibifu wa barabara hiyo inafanyika haraka ili kuandaa maombi ya fedha kwa ajili ya hatua za dharura za kurejesha mawasiliano ya barabara hiyo muhimu.

Serikali inasisitiza umuhimu wa kuimarisha miundombinu ya barabara kuhakikisha mawasiliano na shughuli za maendeleo hayakatiki katika wilaya mbalimbali.

Sauti ya Naibu Waziri wa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Mheshimiwa Zainab Katimba akijibu swali la Mbunge wa jimbo la Hai Saashisha Mafuwe.