Boma Hai FM

Bodaboda Hai wapatiwa elimu

27 March 2025, 8:36 pm

Viongozi wa dini na wadau wakiwa katika mkutano na maofisa wasafirishaji (Bodaboda)

Kutokana na kuwepo kwa ajali nyingi zinazotokana na waendesha bodaboda, Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania Dayosisi ya Kaskazini Jimbo la Hai wamekutana na kuzungumza na waendesha bodaboda hao kwa lengo la kuhakikisha wanabaki salama.

Na Elizabeth Mafie

Maafisa wasafirishaji wametakiwa kuwa waaminifu pamoja na kuepuka mambo maovu,na kuheshimu alama na sheria za  usalama barabarani ili kupunguza ongezeko la ajali za mara kwa mara zinazo hatarisha maisha yao.

Hayo yameelezwa na Mchungaji Mathayo Stanley Mtui ambaye ni Katibu wa idara ya vijana na wanafunzi Dayosisi ya Kaskazini wakati alipo muwakilisha msaidizi wa askofu katika mkutano uliowakutanisha madereva boda boda ama maofisa wasafirishaji wilayani Hai mkoani Kilimanjaro uliofanyika katika usharika wa Hai mjini ( KKKT )Dayosisi ya Kaskazini Jimbo la Hai.

Mchungaji Mathayo amewashauri maofisa wasafirishaji kufanya mambo ya maana ikiwa ni pamoja na Kuwa waaminifu , kuepuka uhalifu jambo ambalo litasababisha kuingia katika mkono wa sheria  pamoja na kuhatarisha Usalama wao na hata wakati mwingine kutumikia kifungo gerezani.

Sauti ya katibu wa idara ya vijana na wanafunzi dayosisi ya Kaskazini jimbo la Hai Mchungaji Mathayo Mtui.

Aidha ameongeza kuwa wanapaswa kuzingatia alama za barabarani kwa lengo la  kuepukana na ajali zitakazo sababisha kupata  ulemavu wa kudumu.

Viongozi wa dini, wadau,na maofisa wasafirishaji wakiwa katika mkutano huo.

Sambamba na hayo amewataka maofisa usafirishaji waliopata fursa ya kuhudhuria mkutano huo kuwa mawakala kwa kutoa Elimu kwa wenzao ili kuwa na madereva boda boda wenye uelewa wa namna ya kujikinga na ajali,kudumisha uaminifu baina yao na wateja.

Kwa upande wake mkuu wa jimbo la Hai mchungaji Binieli Malyo amewataka maofisa Wasafirishaji kujali afya zao lakini pia kujali afya za wateja wao.

Akizungumza katika mkutano huo amesema Ili wateja waendelee kutumia huduma zao yawapasa Kuwa waaminifu kwa kujali Afya zao na za Wateja wao kwa kuepuka Vitu vyote ambavyo ni hatarishi.

Meneja wa Benki Of Afrika Tawi la Moshi (BOA)Mpoki Mwanjara amesema kulingana na kuwa Boda Boda wanatafuta kipato cha kila siku wameona unafuu wao upo katika kuweka malengo ya fedha,kuiheshimu  pamoja na kutunza kwenye akaunti ambazo hazina gharama na zitakazo wapa faida.

Aidha amesema lengo kuu  ni kuhakikisha kuwa  Boda Boda anafikia Malengo yake kwa kupitia kipato anachokipata Kila siku Lakini anajua namna sahihi ya kuhifadhi Fedha, kupitia uhamasishaji wa akaunti mbali mbali mfano BOA ambazo hazina gharama za uendeshaji lakini pia zinawapa faida.

Sauti ya meneja wa bank of Africa tawi la Moshi Mpoki Wanjara.

Maofisa wasafirishaji nao wakapata fursa ya kueleza namna walivyo nufaika na mkutano huo huku waki shukuru kanisa la KKKT Dayosisi ya Kaskazini Jimbo la Hai kwa kushirikiana na wadau mbali mbali kwa kuwathamini na kuona umuhimu wa wao kupata elimu ya usalama  Barabarani.

Sauti ya Bahati Roketi ,dereva boda boda kijiwe cha stand Bomang’ombe.